Ruto sasa atetea ziara zake ng’ambo, asema Kenya inaheshimiwa
RAIS William Ruto amepuuzilia mbali wanaoendelea kumkosoa kuhusu safari zake za mara kwa mara nje ya nchi, akisisitiza kuwa ziara hizo ni sehemu muhimu ya kuimarisha diplomasia ya Kenya na kukuza ushirikiano wa kimataifa unaonufaisha Kenya kimaendeleo.
Akizungumza mjini Mombasa katika hafla yake ya kwanza ya hadhara tangu aliporejea kutoka Ufaransa, Rais Ruto alisema Wakenya wanapaswa kujivunia nafasi ambayo nchi imepata katika jukwaa la kimataifa, ikiwemo kuandaa mikutano mikubwa ya dunia na yeye mwenyewe kualikwa kuwakilisha Afrika katika majukwaa muhimu ya kiuchumi na kisiasa.
Ruto alikuwa Ufaransa kuhudhuria mkutano wa G7, kabla ya kurejea nchini na kufunga rasmi Kongamano la 11 kuhusu Bahari, ambalo kwa mara ya kwanza liliandaliwa barani Afrika, tukio linaloonekana kama mafanikio makubwa kwa diplomasia ya mazingira na bahari.
Alisema mafanikio hayo hayajitokezi kwa bahati, bali ni matokeo ya mipango thabiti ya serikali na juhudi za Wakenya katika kuimarisha nafasi ya nchi kimataifa.
“Haya yote hayatokei kwa bahati au mzaha. Yamepangwa. Ni kwa sababu dunia nzima inaheshimu kazi tunayoifanya kama serikali na kama taifa la Kenya,” alisema Ruto.
Rais aliwahimiza Wakenya kuacha siasa za chuki, propaganda na matusi, akisema taifa linahitaji umoja, mipango na sera madhubuti ili kufanikisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii.
“Naendelea kuwaomba Wakenya wenzangu tujiamini, tuiamini nchi yetu na tuache propaganda, chuki na matusi yasiyo na maana. Tuwe na mipango na sera, ndiyo njia ya pekee ya kupata heshima duniani,” alisema.
Alisema kushiriki kwake katika mkutano wa G7 kulilenga kuwakilisha Afrika katika mijadala ya kimataifa kuhusu mustakabali wa uchumi wa dunia, usalama na ushirikiano wa maendeleo.
Kulingana naye, alitoa msimamo wazi kwamba Afrika inapaswa kuingia katika ushirikiano wa kimataifa kama mshirika sawa, badala ya kuendelea kutegemea misaada.