Habari

2027: Karua afunguka kuhusu upinzani

Na JUSTUS OCHIENG June 21st, 2026 Kusoma ni dakika: 3

HUKU muungano wa upinzani nchini Kenya ukiekea hatua muhimu ya kuchagua mgombea mmoja wa urais atakayemkabili Rais William Ruto katika uchaguzi mkuu wa 2027, mmoja wa vigogo wake ametoa msimamo mkali: hakutakuwa na “uteuzi katika vyumba vya mikutano” wala ugawaji wa vyeo kwa misingi ya maeneo.
Kiongozi wa People’s Liberation Party (PLP), Martha Karua, anasema upinzani lazima ukatae mwelekeo wa kujifungia katika mazungumzo ya faragha na badala yake ukumbatie mchakato wa wazi, wa kisayansi na kidemokrasia unaoakisi matakwa ya Wakenya.
Karua, ambaye ni sehemu ya muungano mpana wa upinzani unaowaleta pamoja aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua, Kalonzo Musyoka (Wiper), Fred Matiang’i (Jubilee), Justin Muturi (DP), Eugene Wamalwa (DAP-K) na Peter Munya (PNU), anasema uaminifu wa muungano huo utategemea jinsi utakavyoshughulikia vita vya uteuzi wa mgombea wa urais.
Msimamo wake unaendana na wito wa Matiang’i na Munya wanaotaka mfumo wa kisayansi kuchagua mgombea wa upinzani, na kupinga vikali sera ya kugawana maeneo ya kisiasa ambayo inahusishwa na Gachagua kupitia chama chake cha DCP, hasa katika Mlima Kenya na Nairobi.
Akizungumza katika mahojiano maalum, Karua alisema mgombea wa upinzani hawezi kuchaguliwa kupitia mazungumzo ya “wanaume wachache mezani”.
“Yeyote anayekuambia tutajifungia chumbani na kutoka na mgombea mmoja amekosa kuelewa. Hatuwezi kuchagua mgombea wa urais katika chumba cha mkutano. Lazima tuzingatie maoni ya wananchi kwa njia ya kisayansi inayoonyesha wanachotaka,” alisema Karua.
Aliongeza: “Hakuna njia nyingine ya kuchagua mgombea zaidi ya mchakato unaopimika na unaoakisi maoni ya wananchi.”
Kuhusu mpango wa kutenga maeneo ya ushawishi wa kisiasa, Karua alisema PLP haikubaliani nao.
“PLP haiungi mkono kugawana maeneo. Vyama lazima vishindane. Demokrasia inataka ushindani na watu wachague,” alisema.
Aidha, alikataa madai kuwa mikutano tofauti ya viongozi wa upinzani inaashiria mpasuko ndani ya muungano huo, akisema kila chama kina haki ya kujipanga na kuimarisha uanachama wake.
Alisema: “Hiyo ni kawaida katika siasa. Vyama vyote vinafanya mikutano yao. Huo si mgawanyiko, ni ushindani wa kirafiki.”
Karua pia alikosoa Serikali ya Kenya Kwanza chini ya Rais Ruto kwa masuala ya matumizi ya fedha za umma, ushuru, mswada wa fedha, ufisadi, ukatili wa polisi, na mchakato wa uboreshaji wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta (JKIA).
Alisisitiza kuwa mradi wowote mkubwa lazima uwe wazi na wenye uwajibikaji ili Wakenya wajue jinsi fedha zao zinavyotumika.
Kuhusu mpango wa kisiasa wa upinzani, Karua alisema muungano huo lazima utegemee wananchi badala ya mikataba ya kisiasa ya nyuma ya pazia.
“Mgombea urais wa upinzani lazima atokane na mchakato unaopimika, si maamuzi ya watu wachache,” alisema.
Alipoulizwa kama angeunga mkono matokeo yoyote ya mchakato huo hata kama asingeibuka mgombeaji, Karua alijibu kwa uthabiti: “Ndio, mradi mchakato ni wa haki na wazi.”
Aliongeza kuwa lengo lake si maslahi binafsi bali mabadiliko ya taifa, akisema upinzani lazima uwasilishe mgombea mmoja mwenye uwezo wa kumshinda Rais Ruto.
Kuhusu hali siasa ukanda wa Mlima Kenya, Karua alisema uongozi haupaswi kuzingatia hesabu za kikabila bali sifa za kitaifa na uungwaji mkono wa wananchi wote.
Alisisitiza kuwa Katiba, hasa Ibara ya 10 na Sura ya Sita ya Maadili ya Uongozi, lazima ziwe msingi wa kuchagua mgombeaji.
“Kiongozi anayehitajika ni mwenye uadilifu, anayeheshimu haki za binadamu na anayezingatia utawala wa sheria,” alisema.
Kuhusu njia ya uteuzi wa mgombea wa upinzani, Karua alisema kura za maoni za kisayansi lazima ziwe sehemu muhimu ya mchakato.
“Utafiti wa kisayansi unaonyesha kama mgombea anakubalika kwa wananchi. Hauwezi kushinda bila kuungwa mkono na watu,” alisema.
Aliongeza kuwa mazungumzo ya kisiasa ni muhimu lakini hayawezi kuchukua nafasi ya sauti ya wananchi.
Kuhusu JKIA, Karua alitaka uwazi kamili katika mchakato wa uboreshaji wake, akisisitiza kuwa mikataba yote ichapishwe kwa umma.
Kuhusu sera za kigeni za Rais Ruto, alisema ziwe na manufaa ya moja kwa moja kwa Wakenya, si idadi ya safari za kimataifa.
Kuhusu fidia kwa waathiriwa wa ukatili wa polisi, Karua alisema fidia pekee haitoshi bila uwajibikaji na kukiri makosa.
“Maisha ya binadamu hayawezi kupimwa kwa pesa,” alisema.
Karua alisema Kenya iko katika wakati muhimu wa maamuzi, akiwataka Wakenya kuchagua viongozi wanaoheshimu Katiba, maisha ya wananchi na rasilimali za umma.