Wetang’ula: Msikubali siasa za ukabila na uhuni
SPIKA wa Bunge la Kitaifa Moses Wetang’ula amewataka Wakenya kukataa siasa za ukabila na vurugu, akisema maendeleo ya taifa yatapatikana kupitia umoja, amani na mshikamano wa kitaifa.
Akizungumza Likoni, Kaunti ya Mombasa, wakati wa harambee ya kuchangisha fedha kwa Shirika la Salute Community-Based Organization (CBO), Wetang’ula alisema Kenya ni kubwa kuliko mtu yeyote na viongozi wanapaswa kuweka maslahi ya taifa mbele ya tofauti za kisiasa na kikabila.
“Hakuna kabila dogo wala kubwa nchini Kenya. Kila jamii ina haki sawa ya kuongoza taifa hili. Tunapaswa kushindana kwa hoja wakati wa uchaguzi, lakini baada ya uchaguzi tufanye kazi pamoja kwa manufaa ya wananchi,” alisema.
Spika huyo alikemea tabia ya baadhi ya wanasiasa wanaodaiwa kuajiri makundi ya wahuni kuvuruga amani nchini.
“Ni jambo la kusikitisha kuona wanasiasa wakitumia vijana kusababisha fujo. Wale wanaotaka wahuni waajiri watoto wao wenyewe badala ya kutumia vijana wasio na hatia,” alisema.
Wetang’ula pia alimpongeza aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga kwa kuweka maslahi ya taifa mbele baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2022.
“Baada ya ushindani wa kisiasa kumalizika, Raila alionyesha kuwa Kenya ni kubwa kuliko mtu yeyote. Hali hiyo ilichangia kuundwa kwa serikali jumuishi inayojumuisha viongozi kutoka pande mbalimbali za kisiasa,” alisema.
Kuhusu uchumi, alisema Kenya iko katika njia ya maendeleo na ustawi chini ya uongozi wa Rais William Ruto.
Naye Spika wa Seneti Amason Kingi alisema eneo la Pwani halitaunga mkono siasa za ukabila kwa kuwa ni nyumbani kwa watu wa jamii mbalimbali.
Waziri wa Madini Hassan Joho alimshukuru Rais Ruto kwa kuhakikisha maeneo yote ya nchi yanapata nafasi sawa ya maendeleo, huku Mbunge wa Likoni Mishi Mboko akimpongeza Wetang’ula kwa ushauri na mwongozo wake wa kisiasa.