Habari za Kitaifa

Wakenya karibu 100,000 hawajui wana HIV hivyo kuzua hofu ya muendelezo wa maambukizi

Na ANGELA OKETCH June 23rd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MKENYA mmoja kwa kila watano anaishi na virusi vya HIV na hajui hilo, kulingana na ripoti mpya ya Baraza la Kitaifa la Kudhibiti Maradhi ya Kuambukizana (NSDCC).

Kati ya watu 1.48 milioni walioambukizwa HIV nchini, asilimia 93 wamethibitisha kuwa na virusi hivyo hatari baada ya vipimo, kwa mujibu wa ripoti hiyo iliyotolewa wiki jana.

Ina maana kuwa watu wapatao 98, 000 hawajagunduliwa hivyo wanaendelea na maisha yao ya kawaida kama vile kwenda kazini, kukimu familia na kujamiiana, huku wamebeba virusi hivyo wasivyoweza kuona na hawajawahi kuelezwa kuvihusu.

Ni Wakenya ambao mfumo haujawahi kuwafahamu kwa sababu hawajakwenda kufanyiwa vipimo.

Idadi ya watu ambao hawajagunduliwa kuwa na virusi ni chanzo kikuu cha maambukizi mapya.

Kaunti zenye idadi kubwa ya watu walioambukizwa HIV na hawajui hali yao ziliandikisha idadi kubwa zaidi ya maambukizi mapya.

“Mtu asiyejua anaugua HIV hawezi kuanza matibabu, hawezi kudhibiti kiwango cha virusi, na hawezi kuwakinga wapenzi wake,” ripoti inasema.

Data iliangazia watu waliofanyiwa vipimo na kujua hali yao lakini hawajaanza matibabu ya kudhibiti virusi (ART), wakitaja woga, unyanyapaa, kunyimwa, gharama ya kusafiri kuchukua dawa, pingamizi kutoka kwa wapenzi wao, au kukosa kufuatilia kati ya kugunduliwa kuwa na virusi na kuhudhuria kliniki.

“Kiwango chao cha virusi hakijadhibitiwa. Uwezo wao wa kuambukiza unakaribia wa mtu ambaye hajawahi kamwe kupimwa,” inaonya ripoti.

Hali miongoni mwa watoto inahofisha mno. Zaidi ya nusu ya watoto wote walio chini ya umri wa miaka mitano wenye HIV hawapokei matibabu.

Miongoni mwa watoto 12,912 wenye umri kuanzia sufuri hadi miaka minne wanaoishi na HIV, ni 5,876 pekee wanatumia ART, sawa na asilimia 46.

Kwa watoto wenye umri kati ya miaka mitano na tisa, zaidi ya mmoja miongoni mwa kila watatu hapokei matibabu.

Ripoti hiyo imemulika kaunti tisa zilizoathirika zaidi ambapo idadi ya watu wasiojua hali zao ni takriban asilimia tano zaidi.

Marsabit, Wajir, Mandera, Garissa na Samburu, kiwango cha maambukizi ya HIV ni cha chini lakini watu hawafikiwi kwa sababu ya eneo hilo kuwa la mashinani, upungufu wa vituo vya afya, pingamizi za kitamaduni dhidi ya vipimo na unyanyapaa.

Mandera, Wajir na Garissa, wanaume wanaepuka kupimwa katika kile data inaeleza kuwa “kaunti zenye unyanyapaa wa kiwango cha juu” na vifo vyao vinajitokeza katika idadi ya vifo inayozidi kupanda katika kaunti hizoo.

Kilifi, Kericho, Nandi, Laikipia na Busia, idadi kubwa ya watu wanaishi bila kujua hali zao, hali inayojitokeza kwenye idadi ya maambukizi mapya.