Maadhimisho: Kesi nyingi za maandamano ya Gen Z bado hazijaona mwangaza
MIAKA miwili baada ya maandamano ya vijana wa Gen Z yaliyotikisa nchi wakipinga Mswada wa Fedha wa 2024, kesi nyingi za mauaji, ukiukaji wa haki za binadamu na madai ya matumizi mabaya ya mamlaka na polisi bado hazijashughulikiwa.
Licha ya ahadi za kuwawajibisha waliohusika, ni kesi tatu pekee za jinai zinazohusu vifo 62 vilivyohusishwa na polisi wakati wa maandamano hayo zimefikishwa mahakamani, huku uchunguzi wa visa vingine ukiendelea.
Hali hiyo imezidishwa na uchunguzi mpya kuhusu vifo vilivyotokea wakati wa maandamano ya kumbukumbu ya Gen Z na maandamano ya Sabasaba mwaka 2025, jambo linalozua maswali kuhusu kasi ya utoaji wa haki.
Kulingana na Mamlaka Huru ya Kusimamia Utendakazi wa Polisi (IPOA), uchunguzi wa vifo 62 vya mwaka 2024 ulisababisha kesi tatu kufikishwa mahakamani baada ya kukidhi kiwango cha ushahidi kinachohitajika.
Aidha, faili tatu zimewasilishwa kwa Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (ODPP) kwa ushauri, moja iko katika ukaguzi wa kisheria wa IPOA, nne zilifungwa baada ya tathmini ya ndani, tano zilifungwa kufuatia ushauri wa ODPP, huku kesi 46 zikiendelea kuchunguzwa.
IPOA ilisema ucheleweshaji huo unatokana na uchunguzi tata unaohitaji ripoti za kitaalamu, uchambuzi wa risasi, uchunguzi wa Mwanakemia Mkuu wa Serikali na ushahidi wa kutosha kabla ya mashtaka kuidhinishwa.
“Kesi tatu zilizo mahakamani ni zile ambazo ushahidi wake ulikidhi viwango vya uchunguzi na mashtaka, hivyo kuruhusu kesi ya jinai kuanza,” ilisema IPOA.
Mamlaka hiyo pia ilisema imeanza uchunguzi kuhusu vifo 27 vilivyotokea wakati wa maandamano ya kumbukumbu ya Gen Z ya Juni 2025.
Kesi moja tayari iko mahakamani huku nyingine 26 zikiendelea kuchunguzwa.
Aidha, IPOA imenakili vifo 38 vilivyotokea wakati wa maandamano ya Sabasaba ya Julai 2025. Uchunguzi wa kesi mbili umekamilika ndani ya mamlaka hiyo huku 36 zikiendelea.
Kwa jumla, IPOA sasa inachunguza vifo 127 vinavyohusishwa na mawimbi hayo matatu ya maandamano.
Miongoni mwa kesi zinazofuatiliwa kwa karibu ni ile ya mauaji ya Rex Masai, mmoja wa waandamanaji wa kwanza kuuawa mwaka 2024. Afisa wa Polisi Isaiah Ndumba Murangiri anahusishwa na mauaji hayo.
Kesi nyingine inayovuta hisia ni ile ya Konstebo Klinzy Baraza Masinde anayeshtakiwa kwa kumpiga risasi muuzaji wa barakoa Boniface Kariuki wakati wa maandamano ya Juni 2025.
Mbali na kesi za jinai, Mahakama Kuu bado inashughulikia kesi kadhaa za kikatiba zilizowasilishwa na watu binafsi na mashirika ya kutetea haki za binadamu.
Miongoni mwa kesi hizo ni ya Chama cha Wanasheria Kenya (LSK), kinachopinga madai ya serikali kupata na kutumia data za simu za waandamanaji bila amri ya mahakama.
Pia kuna kesi ya Katiba Institute inayopinga kufungwa kwa barabara zinazoingia katikati mwa jiji la Nairobi wakati wa maandamano ya Juni 2025, ikisema hatua hiyo ilikiuka haki ya kukusanyika na kusafiri kwa uhuru.
Kesi nyingine zinahusu madai ya kukamatwa kiholela kwa mamia ya waandamanaji, kutoweka kwa baadhi ya wanaharakati, matumizi ya Jeshi la Ulinzi la Kenya (KDF) wakati wa maandamano na kuhifadhi miili ya watu waliodhaniwa kuhusishwa na maandamano hayo kabla ya kuzikwa.