Safari yake baada ya kubainika kuugua ugonjwa wa lupus
AKIWA shuleni alijulikana kuwa miongoni mwa wanafunzi waliotia fora masomoni na kuwa kati ya watatu bora kwenye kila mtihani.
Hatua hiyo ilimpa motisha, Purity Nkatha kuyapenda sana masomo yake.
Ila wakati janga la corona liliporipotiwa humu nchini na wanafunzi wakaruhusiwa kuenda nyumbani kama njia moja ya kudhibiti kuenea kwa ugonjwa huo, Purity ambaye pia alikuwa nyumbani wakati huo, anasema kuwa alianza kupata maumivu ya ugonjwa ambao hakuufahamu moja kwa moja.
“Jioni hiyo tulikuwa nyumbani tukitazama runinga. Ghafla nilianza kuhisi kisunzi, dakika chache baadaye sikuwa nasikia sauti yoyote. Ilikuwa vigumu kuelewa kilichokuwa kikiendelea kwenye ulimwengu wangu maanake kabla ya tukio hilo, afya yangu ilikuwa salama kabisa. Singetarajia kuwa ningeugua,” anasimulia Purity.
Asubuhi iliyofuata, Purity anasema kuwa maumivu yalimzidi na akapelekwa hospitalini ambapo alilazwa siku tatu. Pia aligunduliwa kuwa na shinikizo la juu la damu pamoja na mafindofindo.
“Katika muda huo mchache wa kuugua nilikuwa mnyonge sana kwenye mwili, singesimama bila usaidizi. Shinikizo la juu la damu lilidhibitiwa lakini tuliambiwa kuwa mafindofindo yalihitaji upasuaji katika hospitali tofauti,” anasema.
Purity anaeleza kuwa baadaye alifanyiwa upasuaji wa mafindofindo lakini maumivu yalizidi. Jamaa wake nao walianza kumtafutia matibabu maalum kwenye hospitali za rufaa.
“Ilituchukua takriban mwaka mmoja kutibu dalili tofauti za maumivu mwilini mwangu kabla madaktari kugundua kuwa nilikuwa naugua ugonjwa wa lupus. Pindi tu nilipopatikana kuwa naugua ugonjwa wa lupus, niliwekwa kwenye matibabu mara moja,” anasema.
Baada ya kuanza matibabu ya ugonjwa huo wa lupus, Purity anasema kuwa madaktari walimruhusu kurudi shuleni. Alitumia muda uliosalia kujiandaa kwa mtihani wake wa kidato cha nne ambao alifaulu kuufanya na kupata alama ya B-.
“Ilikuwa furaha kwangu kupita mtihani wangu maana niliufanya mwili wangu ukiwa umefura kutokana na ugonjwa wa lupus. Nilipata motisha ya kusomea taaluma ya uuguzi ili kuelewa zaidi ugonjwa huo,” anaeleza.
Alipofuzu mwaka jana kama muuguzi, Purity alifurahi sana kutimiza ndoto hiyo. Safari yake ni ushuhuda kuwa, mtu anayeugua ugonjwa wa lupus anawezaishi maisha ya kawaida akipata matibabu na usaidizi.
“Dawa za lupus ni ghali sana na mara nyingi nategemea wasamaria na marafiki kunichangia pesa za kununua hizo dawa maanake nazitumia kila siku. Kupata ajira kama muuguzi kutanisaidia sana kugharamia matibabu hayo na pia kuwahudumia wagonjwa wengine wa lupus,” anasema muuguzi Purity akiwa nyumbani kwao Rwarera-Ruiri, Kaunti ya Meru,
Ulimwengu ulipoadhimisha siku ya lupus mwezi jana, wito ulikuwa kuweka mwanga kwenye dalili fiche, zile zisizoeleweka na maumivu makali ya ugonjwa huu kwani watu wengi kwenye jamii, bado hawana ufahamu wa kutosha kuhusu ugonjwa wa lupus.
“Kabla nigunduliwe kuugua ugonjwa wa lupus, watu wengi walikuwa wakiniuliza kama ni uchawi. Lakini hata mimi sikuwa na wakasirikia maanake pia mimi nilikuwa najiuliza hayo hayo maswali. Nilipata sana afueni nilipojua jina la ugonjwa huu maanake hapo ndio sasa watu pia walianza kunipa ushauri nasaha,” anasema Purity.
Kwa sasa muuguzi Purity amejiunga na wagonjwa wengine wa lupus kutoa hamasisho kwa umma. Wito wake kwa serikali ni kupunguza gharama za dawa za lupus ili kurahisisha safari ya matibabu ya ugonjwa huo ambao hauna tiba.
“Kuenda kwenye hospitali imekuwa sehemu ya maisha yangu tangu nilipogunduliwa kuwa na ugonjwa wa lupus. Wakati mwingine napata maumivu usiku na hospitali iko mbali. Hizo zote ni gharama za maisha yangu sasa. Bila ajira na usaidizi wa jamaa na marafiki, inakuwa ni safari ngumu sana ambayo pia inatatiza hata afya ya akili,” anasema Purity.
Dalili za ugonjwa wa lupus ni kama uchovu wa kupindukia, maumivu kwenye viungo vya mwili, vipele kwenye ngozi, upungufu wa damu na kuvimba mwili.
Dkt Philip Simani, anasema kuwa ugonjwa huo unagunduliwa kwa kuangazia historia na matokeo mbalimbali ambayo pia yanapitia vipimo kadhaa za hali ya juu kwenye maabara. Anaongeza kuwa madaktari hutumia muda mwingi kubaini kuwa vipimo vile si vya dalili za magonjwa mengine yanayofanana na ugonjwa wa lupus kabla mgonjwa kuambiwa kuwa anaugua ugonjwa huo.
“Ugonjwa wa lupus ni mara kumi zaidi miongoni mwa wanawake ikilinganishwa na wanaume. Kawaida lupus inakuwa miongoni mwa wanadamu walio kati ya umri wa miezi kumi na minane hadi miaka themanini,” anasema Dkt Simani.
Pia anasema kuwa wanawake wanaougua ugonjwa wa lupus wamo kwenye hatari ya kupoteza ujauzito au kujifungua mapema kabla ya wiki 40 za ujauzito kukamilika.
Wanawake walio na lupus wana uwezo wa kubeba ujauzito na kujifungua lakini ni muhimu sana kwa wanawake hao kupata ushauri kabla wapate ujauzito ili kuwahamasisha endapo kuna uwezekano kupata matatizo wakati wa ujauzito miongoni mwa changamoto zingine za ujauzito,” anashauri Dkt Simani.
Aidha anaeleza kuwa matatizo wakati wa ujauzito yameripotiwa kuathiri mwanamke anayeugua ugonjwa wa lupus kama vile kudhoofika kwa figo, mvilio wa damu, matatizo ya mifupa na kuwa kwenye hatari ya kupata magonjwa mengine kama vile ugonjwa wa kisukari.
“Tunaanza kuelewa zaidi kuhusu sababu zinazosababisha ugonjwa wa lupus. Elimu ya vinasaba inaonekana kuwa na nafasi kuu miongoni ni mwa wagonjwa wengi wa lupus. Mazingira pia kama vile jua kali huzidisha ugonjwa huo na ndio maana ni vyema mgonjwa wa lupus aepuka jua kali akiwa nje ya nyumba,” anashauri Dkt Simani.
Ingawa hakuna matibabu ya ugonjwa wa lupus kufikia sasa, Dkt Simani anasema kuwa wanasayansi wamepiga hatua ili kuwasaidia wagonjwa kuishi maisha ya kawaida.
“Udhibiti bora wa ugonjwa wa lupus unahusisha ushirikiano wa karibu na wa mara kwa mara kati ya mgonjwa wa lupus na daktari wake pamoja na wataalamu wa matibabu ili kuhakikisha kuwa wagonjwa wa lupus wanapata huduma bora zaidi za matibabu. Miaka ya karibuni, tunaona kuwa hatua hii inarekodi maisha marefu miongoni mwa wagonjwa wa lupus walio kwenye matibabu,” anaongeza Dkt Simani.