Habari

Siasa za ubabe: Ruto na Gideon Moi wazozana

Na JUSTUS OCHIENG Na MOSES NYAMORI June 28th, 2026 Kusoma ni dakika: 4

MIEZI kadhaa baada ya Rais William Ruto na mwenyekiti wa Kanu Gideon Moi kuonekana wakisalimiana kwa bashasha huko Kabarak na kuahidi kushirikiana chini ya serikali jumuishi, viongozi hao wawili mashuhuri kutoka Bonde la Ufa wamejikuta tena katika vita vya wazi vya kisiasa.

Kauli kali zimekuwa zikirushwa kutoka pande zote, hali iliyofufua uhasama wa kisiasa uliodumu kwa zaidi ya miongo miwili. Wachambuzi wa siasa wanasema mgogoro huo hauhusu tofauti za kibinafsi pekee, bali ni mapambano kuhusu uhalali wa kisiasa, urithi wa mamlaka na vita visivyokwisha kuhusu urithi wa kisiasa wa hayati Rais Daniel arap Moi.

Kwa mujibu wa wachambuzi hao, huu ni mkasa wa ulezi wa kisiasa, urithi, uaminifu, tamaa ya uongozi na kile ambacho wengine hukitafsiri kama usaliti.

Ni simulizi ya jinsi uhusiano wa karibu kati ya Dkt Ruto, aliyekuwa mmoja wa wanafunzi wa kisiasa wa Moi, na Gideon, kitinda mimba wa rais huyo wa zamani, ulivyogeuka na kuwa ushindani mkubwa unaoendelea kuathiri siasa za Bonde la Ufa na ambao huenda ukaathiri uchaguzi mkuu wa Agosti 10, 2027.

Kwa muda mrefu, safari ya kisiasa ya Dkt Ruto ilikuwa imefungamana kwa karibu na familia ya Moi. Hayati Moi alimtambua akiwa kijana, akamlea kisiasa na kumfungulia milango iliyomgeuza kutoka mwanaharakati wa Chuo Kikuu cha Nairobi hadi kuwa mmoja wa viongozi chipukizi waliotikisa chama cha Kanu.

Kwa upande mwingine, Gideon Moi alikulia katikati ya mamlaka. Kama mtoto wa rais wa pili wa Kenya, wengi walimwona kuwa mrithi wa kisiasa wa familia ya Moi na mtu ambaye angeendeleza ushawishi wa Kanu katika Bonde la Ufa. Hata hivyo, mambo hayakuenda kama ilivyotarajiwa.

Kwa miaka mingi viongozi hao walikuwa ndani ya mzunguko mmoja wa kisiasa lakini kila mmoja akiwa na msingi tofauti wa uhalali. Dkt Ruto alijijengea jina kupitia juhudi zake binafsi, uwezo wa kupanga siasa na ushawishi wa mashinani, ilhali Gideon alibeba uzito wa jina la familia, historia na urithi wa kisiasa wa baba yake.

Mvutano wao wa sasa umeibua tena swali ambalo limekuwepo tangu Moi alipostaafu mwaka wa 2002: Ni nani aliyerithi kweli ufalme wa kisiasa wa Daniel arap Moi?

Hatua kubwa ya Dkt Ruto kisiasa ilikuja mwaka wa 1992 alipojiunga na kundi la Youth for Kanu ’92 (YK’92), lililoanzishwa kusaidia kampeni za Moi katika uchaguzi wa kwanza wa vyama vingi.

Ruto alijitofautisha kwa nidhamu, uwezo wa kupanga shughuli za kisiasa na umahiri wa kuhamasisha wananchi mashinani. Sifa hizo zilimvutia Moi, ambaye alimpa nafasi ya kugombea ubunge wa Eldoret North kupitia Kanu mwaka wa 1997 licha ya upinzani kutoka kwa baadhi ya viongozi wa chama. Alishinda uchaguzi huo akiwa na umri wa miaka 30 na kuanza safari yake ya kupanda ngazi za kisiasa hadi kuwa Naibu Rais na baadaye Rais.

Tofauti na Ruto, Gideon hakulazimika kupigania nafasi yake ya kwanza kisiasa. Alizaliwa katika familia iliyokuwa madarakani, lakini Moi hakumwingiza haraka kwenye siasa za uchaguzi. Alisubiri hadi mwaka wa 2002, Gideon aliposhinda ubunge wa Baringo Central na kuchukua nafasi ya baba yake katika eneo lililokuwa kitovu cha nguvu za kisiasa za familia hiyo kwa miongo kadhaa.

Ushindi huo uliibua matarajio kwamba angepewa jukumu la kulinda urithi wa kisiasa wa familia ya Moi baada ya baba yake kung’atuka. Lakini wakati huo tayari kulikuwa na mwanasiasa mwingine wa Kalenjin aliyekuwa akipaa kwa kasi katika Bonde la Ufa — William Ruto.

Moi alipomteua Uhuru Kenyatta kuwa mrithi wake mwaka wa 2002, viongozi wengi wakuu wa Kanu walikihama chama. Hata hivyo, Ruto alibaki mwaminifu na kufanya kampeni kwa nguvu kumsaidia Uhuru. Ingawa Kanu ilipoteza mamlaka kwa mara ya kwanza tangu uhuru, uaminifu huo ulimjengea heshima kubwa Bonde la Ufa.

Katika uchaguzi wa 2007, Ruto aliunga mkono Raila Odinga kupitia ODM huku Gideon akiunga mkono Rais Mwai Kibaki. Ushindani wao haukuwa wa kibinafsi hadi mwaka wa 2013, Ruto alipoungana na Uhuru Kenyatta na kuwa Naibu Rais.

Uchaguzi wa mwaka wa 2022 uliamua mwelekeo wa ushindani wao. Ruto aliongoza muungano wa Kenya Kwanza na kushinda urais, huku Gideon akiunga mkono Raila Odinga. Mbali na Raila kushindwa, Gideon pia alipoteza kiti chake cha Seneta wa Baringo kwa mgombea wa UDA William Cheptumo. Matokeo hayo yaliashiria kupungua kwa ushawishi wa kisiasa wa familia ya Moi katika Bonde la Ufa.

Hata hivyo, mwaka wa 2025 viongozi hao walionekana kupatana baada ya Rais Ruto kuunda serikali jumuishi. Gideon alijiondoa katika uchaguzi mdogo wa useneta wa Baringo baada ya kukutana na Rais, ambaye baadaye alimtembelea Kabarak na kutangaza kuwa walihitaji kushirikiana kwa manufaa ya taifa.

Lakini maelewano hayo hayakudumu. Viongozi wa Kanu wanasema ahadi mbalimbali walizopewa hazikutimizwa, hali iliyozua malalamiko ndani ya chama.

Wiki hii uhusiano huo ulivunjika waziwazi baada ya Rais Ruto kumshutumu Gideon kwa kile alichokiita usaliti wa kisiasa na kutumia vyombo vya habari vinavyohusishwa na familia ya Moi kueneza propaganda dhidi ya serikali.

Kanu ilijibu kupitia Katibu Mkuu George Wainaina, aliyedai kuwa upande wa serikali haukutimiza makubaliano yaliyofikiwa wakati wa mazungumzo ya maridhiano. Alisema  jinsi Standard Group imekuwa ikiripoti serikali haikuwa sehemu ya makubaliano hayo kwa kuwa kampuni hiyo ni taasisi ya kibinafsi yenye wanahisa wengi.

“Tuliyokubaliana hayakutekelezwa. Hakukuwa na nia njema kutoka upande wao. Hawakutimiza ahadi walizotupa,” alisema Bw Wainaina.

Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Kanu, Bw Manasse Nyainda, alisema chama hicho kilitimiza wajibu wake baada ya kujiondoa kwenye uchaguzi mdogo wa useneta wa Baringo.

“Tulijiondoa kwenye uchaguzi huo kufuatia ombi lake. Hatukuweka masharti yoyote wala kudai chochote. Ni yeye aliyetoa ahadi, hivyo ilikuwa jukumu lake kuhakikisha amezitimiza,” alisema.

Wakili Chris Omore anaamini viongozi hao wawili wana deni la kisiasa kwa hayati Moi.

“Bila ulezi na mwongozo wa Moi, huenda safari ya kisiasa ya William Ruto ingekuwa tofauti kabisa. Vivyo hivyo, bila urithi wa kisiasa wa Moi, Gideon asingekuwa kiongozi asiye na mpinzani ndani ya Kanu. Kwa namna fulani, mtu huyo mmoja ndiye aliyeunda misingi ya safari za kisiasa za viongozi hawa wawili,” alisema.

Naye Profesa Gitile Naituli wa Chuo Kikuu cha Multimedia anasema mzozo unaoshuhudiwa sasa ni mwanzo wa mapambano ya uchaguzi mkuu wa 2027.

“Kile tunachoshuhudia sasa ni hatua za mwanzo za uwanja wa kisiasa wa 2027. Kila kauli, kila mzozo na kila muungano unaojengwa sasa unapaswa kutazamwa kupitia muktadha huo,” alisema.