Kauli ya Oburu kwamba hatabeba yeyote mgongoni iandamane na vitendo
KAULI ya Kinara wa ODM, Dkt Oburu Oginga kuwa hakuna mwanasiasa atakayening’inia koti lake katika uteuzi wa chama na kuwa kutakuwa na uteuzi huru inastahili kuandamana na vitendo.
Dkt Oginga mnamo wikendi alisema kuwa hakuna kiongozi ambaye atapendelewa na kupewa tikiti huku akisema utendakazi wa kiongozi husika ndio utaamua iwapo atachaguliwa au la.
Kinaya ni kwamba baada ya kutoa matamshi hayo, seneta huyo wa Siaya alimtaka Mbunge wa Ugenya David Ochieng’ wa MDG arejee ODM ili awe gavana wa Siaya.
Hii ni licha kuwa baadhi ya viongozi ndani ya ODM kama aliyekuwa Mbunge wa Rarieda Nicholas Gumbo, wametangaza kuwa wanalenga kutumia chama hicho kuwania ugavana.
Dkt Oginga atatumia msingi gani kuwahakikishia wawaniaji kuwa uteuzi wa chama utakuwa huru ilhali mwenyewe anawaalika waliohepa warejee chamani kwa ajili ya kupewa uongozi.
Mbona hakusema kuwa Bw Ochieng’ arejee ODM na apambanie tikiti na Bw Gumbo, Naibu Gavana Oduol Denge pamoja na viongozi wengine wanaosaka ugavana?
Kauli ya Dkt Oginga itakuwa tu ya kuwafurusha wawaniaji iwapo chama hakitaweka msingi imara wa kuhakikisha uteuzi wa ODM hauvurugwi.
ODM ina mizizi yake kisiasa katika kila eneo nchini lakini iwapo hakutakuwa na uteuzi huru, kila kitu kitaenda tenge na wafuasi kupoteza imani hasa wakati huu ambapo Raila Odinga hayuko.
Kwanza, Dkt Oginga, 83 mwenyewe ametangaza kuwa atatetea kiti cha useneta wa Siaya na aliyekuwa Gavana Cornel Rasanga pia tayari ametangaza kuwa analenga kiti hicho.
Je, mwenyewe yuko tayari kuridhika na matokeo hata akishindwa?
Haya ni maswali mazito ambayo wafuasi wa chama lazima wajiulize kwa sababu kusema tu kuwa uteuzi utakuwa huru bila vitendo si jambo lenye mashiko.
Kama kuna eneo ambalo ODM inastahili kujikuna kichwa zaidi basi ni ugavana kwenye ngome yake ya Luo Nyanza.
Matokeo ya mchujo wa ugavana Kisumu, Migori, Homa Bay na Siaya huenda yakaamua mustakabali wa ODM kwenye ngome yake.
Gatuzi la Kisumu lina viongozi sita waliochaguliwa ambao wote wanasaka tikiti ya ugavana kupitia ODM.
Hao ni Mbunge wa Kisumu ya Kati Dkt Joshua Oron, Seneta Tom Ojienda, Mbunge wa Nyakach Aduma Owuor, Mbunge wa Kisumu Mjini Magharibi Rosa Buyu, Naibu Gavana Mathews Owili na Mbunge Mwakilishi wa Kike Ruth Odinga.
Je, ODM itatumia mbinu gani kuhakikisha kuwa inasimamia uteuzi huru na vigogo hawa wote wanaridhika na uteuzi ili wanaoshindwa wasielekee debeni kama wagombeaji huru?
Kwenye Kaunti ya Migori Gavana Ochillo Ayacko na Mbunge wa Uriri Mark Nyamita nao wameapa kuwa kila moja lazima afike debeni kupitia ODM.
Bw Nyamita amekuwa akisisitiza kuwa mchujo wa ODM lazima uwe huru akidai uungwaji mkono ambao ameupata unaonyesha kuwa atashinda ugavana.
Kwenye Kaunti ya Homa Bay mchuano mkali unatarajiwa kati ya Gavana Gladys Wanga na aliyekuwa Naibu Gavana Oyugi Magwanga.
Uzito wa majina hasa wale wanaosaka ugavana unaonyesha tu kuwa chama kisipomakinikia uteuzi huru, basi kitasalia kimevurugwa na kigae kiasi cha kupoteza umaarufu.
Michujo ya ODM huwa imejaa fujo na ni vyema kila maandalizi yawekwa ili wananchi na viongozi waridhike na uteuzi ndipo chama kiwe imara.