Watoto 6 kutoka Kibra kushuhudia robo fainali ya Kombe la Dunia nchini Marekani
MAKINDA sita kutoka mtaa wa Kibra, Nairobi, wamepata nafasi ya kipekee ya kuiwakilisha Kenya katika tamasha la kimataifa la vijana la Festival 26 litakalofanyika jijini Boston, jimbo la Massachusetts nchini Marekani kuanzia Julai 5 hadi 13.
Kilele cha safari hiyo kitakuwa kushuhudia mechi ya robo fainali ya Kombe la Dunia, mechi zitakazochezwa kati ya Julai 9 na 11 katika miji ya Boston, Los Angeles, Miami na Kansas City.
Chipukizi hao, wanaojumuisha wavulana watatu na wasichana watatu wenye umri wa kati ya miaka 13 na 16, walichaguliwa kupitia shirika la Carolina for Kibera (CFK Africa) baada ya mchujo mkali uliowashirikisha zaidi ya watoto 500 kutoka mitaa duni ya Kibra, Mathare, Mukuru kwa Njenga, Viwandani, Kangemi na Kiandutu.
Tamasha hilo, linaloandaliwa na Boston Scores kwa ushirikiano na Sport dans la Ville za Marekani, litawakutanisha zaidi ya vijana 400 kutoka mataifa 24 kwa wiki moja ya michezo, mafunzo ya uongozi, kujifunza tamaduni na maendeleo ya jamii.
Kenya itashiriki kwa mara ya kwanza katika tamasha hilo pamoja na wajumbe kutoka mabara matano. Afrika pia itawakilishwa na Youth Sport Uganda (Uganda), Tibu Africa (Morocco), Fafali Organisation (Ghana) na Oasis Reach for Your Dreams (Afrika Kusini).
Mbali na kushiriki mashindano ya soka na wachezaji kutoka mataifa mbalimbali, vijana hao watapata mafunzo ya uongozi, kushiriki shughuli za kubadilishana tamaduni na kutembelea maeneo muhimu ya kihistoria, kisayansi na kitamaduni jijini Boston.
Miongoni mwa waliochaguliwa ni Erick Manchang, 15, mwanafunzi wa Shule ya Ngei Junior na beki wa Millennium Soccer Academy.
Faridah Mahmoud, 14, pia alichaguliwa na ni mwanafunzi wa Shule ya Msingi ya State House, alisema anatamani kukutana na vijana kutoka mataifa mbalimbali na kutazama mechi ya Kombe la Dunia akiwa uwanjani.
Wengine ni pamoja na Harriet Sandra Achieng (Olympic Junior School), Nigel Mali (St. Elizabeth Primary School), Valary Ayuma (Rungiri High School), na Nehemiah Ongori Ayora (Gifted Hands Educational Center).