Habari za Kitaifa

DPP: Upo ushahidi kifo cha Ojwang kilipangwa mikononi mwa polisi

Na SAM KIPLAGAT July 21st, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MKURUGENZI wa Mashtaka ya Umma (DPP) Renson Ingonga ameambia Mahakama Kuu kuwa upande wa mashtaka utawasilisha ushahidi kuonyesha kuwa kifo cha mwalimu na mwanablogu Albert Ojwang kilipangwa.

Bw Ingonga anasema mauaji hayo yalipangwa Bw Ojwang akiwa mikononi mwa polisi, wala si ajali kama ilivyodaiwa awali.

Akitoa hoja wakati wa kuanza kwa kesi katika Mahakama Kuu ya Kibera jana, mwendesha mashtaka mkuu msaidizi Gikui Gichuhi alisema ushahidi utaonyesha jinsi maafisa wa polisi walipanga kipigo kilichosababisha kifo cha Ojwang kisha wakajaribu kuficha ukweli.

Aliyekuwa Kamanda wa Kituo cha Polisi cha Central, Samson Tallam, anakabiliwa na mashtaka ya mauaji pamoja na maafisa wa polisi James Mukhwana na Peter Kimani.

Wengine walioshtakiwa ni raia watatu, John Ngige Gitau, Jim Ambao na Brian Njue, waliokuwa wakizuiliwa katika seli moja na Bw Ojwang.

Bw Gichuhi alisema ushahidi wa kimatibabu utaonyesha kuwa Ojwang alipata majeraha mengi mwilini yaliyosababishwa na kupigwa, kinyume na madai ya awali ya polisi kwamba alijijeruhi kwa kujigonga ukutani.

Upande wa mashtaka pia ulisema utawasilisha ushahidi unaodaiwa kuonyesha kulikuwa na juhudi za kuharibu uchunguzi, ikiwemo kufutwa kwa picha za kamera za usalama (CCTV) katika kituo cha polisi.

Bw Ojwang alikamatwa nyumbani kwake Kakoth, Kaunti ya Homa Bay, Juni 7, 2025 na maafisa wa DCI kufuatia malalamishi kuhusu chapisho la mitandaoni lililomlenga na Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi Eliud Langat.

Baadaye alihamishwa hadi Kituo cha Polisi cha Central, Nairobi, ambako alifariki akiwa rumande.

Ripoti ya uchunguzi wa maiti ilibaini alikuwa na majeraha mabaya kichwani, shingoni na sehemu nyingine za mwili, huku wataalamu wakihitimisha kuwa yalitokana na kushambuliwa na si kujidhuru.

DPP anasisitiza kuwa washtakiwa wote sita walihusika katika mauaji hayo, huku uchunguzi ukiendelea chini ya Mamlaka Huru ya Kutathmini Utendakazi wa Polisi (IPOA).