Mwanamume apigwa risasi Siaya wakazi wakipinga kiwanda cha nyuklia
MTU mmoja amelazwa hospitalini baada ya kupigwa risasi mguuni vurugu zilizozuka katika mkutano wa uhamasishaji kuhusu mradi wa kujenga kiwanda cha nyuklia cha thamani ya Sh1 trilioni katika eneo la Central Sakwa, Bondo, Kaunti ya Siaya, Ijumaa alasiri.
Mkutano huo uliofanyika katika Kituo cha Biashara cha Ka’John ulihudhuriwa na maafisa wa KenGen, Shirika la Nishati na Umeme wa Nyuklia na Mbunge Gideon Ochanda.
Waliokuwa wakielezea mradi huo kwa wakazi kabla ya vurugu kuzuka.
David Otieno Mboya, mchimbaji mdogo wa madini kutoka kijiji cha Lenya, alisema hakuwa miongoni mwa waliohudhuria mkutano huo bali alikuwa akirejea nyumbani kutoka kazini alipopigwa risasi.
“Nilikuwa napita karibu na eneo la mkutano vurugu zilipoanza. Wakazi walikuwa wakirusha mawe huku polisi wakifyatua risasi. Ghafla nilihisi maumivu makali kwenye mguu wa kushoto na nikagundua nimepigwa risasi,” alisema.
Alisema hajui iwapo alipigwa risasi na walinzi wa Mbunge Ochanda au maafisa wa polisi waliokuwa eneo hilo.
Wasamaria wema walimkimbiza katika Hospitali ya Nango kabla ya kuhamishwa hadi Hospitali ya Bondo.
Otieno alisema wakazi wengi wanapinga mradi huo kwa sababu utawalazimu kuhamishwa kutoka makazi yao ya muda mrefu.
Mkazi mwingine, Otieno Ombok, alisema NuPEA imepuuza maswali ya jamii kuhusu usalama, fidia na uhamishaji wa wakazi, jambo lililosababisha hasira.
Kamanda wa Polisi wa Bondo Peter Leparsare, alisema hakuna aliyekuwa ameripoti rasmi kupigwa risasi kufikia Ijumaa usiku, lakini alithibitisha kuwa polisi walifyatua risasi angani kutawanya umati baada ya mzozo kati ya wakazi na walinzi wa mbunge.
Mradi huo ulihamishwa kutoka Kilifi hadi Siaya baada ya kupingwa na wakazi wa Kilifi.
Serikali inapanga kuongeza uzalishaji wa umeme nchini kwa kati ya megawati 3,000 na 6,000 kupitia mradi huo.
Gavana wa Siaya James Orengo amesisitiza kuwa mafanikio yake yatategemea ushirikishaji wa wananchi, uwazi na ridhaa kamili ya jamii itakayoathirika.