Habari za Kitaifa

Kibarua Upinzani kuamua gani kali kati ya Kalonzo-Matiang’i, Kalonzo-Sifuna, Sifuna-Kalonzo

Na JUSTUS OCHIENG July 30th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

UPINZANI sasa unakabiliwa na mtihani mkubwa zaidi kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027. Baada ya kuonekana kukubaliana kuhusu haja ya kuungana dhidi ya Rais William Ruto, sasa viongozi wake wanapaswa kuamua nani atapeperusha bendera ya urais na nani atakuwa mgombea mwenza.

Baada ya aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua kuondolewa rasmi katika kinyang’anyiro cha urais kufuatia kutimuliwa afisini, mjadala umehamia kwa miungano minne inayoweza kuundwa.

Wachambuzi wa kisiasa na viongozi wa upinzani sasa wanazungumzia uwezekano wa tiketi za Kalonzo-Matiang’i, Matiang’i-Kalonzo, Kalonzo-Sifuna au Sifuna-Kalonzo.

Hadi majuzi, kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka na aliyekuwa Waziri wa Usalama wa Ndani Fred Matiang’i walionekana kuwa wagombeaji wakuu wa kuwania urais kupitia muungano huo.

Hata hivyo, Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna ametikisa hesabu hizo baada ya kura ya maoni ya TIFA kumweka mbele ya Kalonzo na Matiang’i kwa mara ya kwanza.

Licha ya mabadiliko hayo, jambo moja linaonekana wazi katika mazungumzo yote ya upinzani; Kalonzo bado anaonekana kuwa nguzo muhimu, iwe kama mgombea wa urais au mgombea mwenza.

Wachambuzi wanasema kuibuka kwa Sifuna na vuguvugu la Linda Mwananchi kumebadilisha kabisa mizani ya kisiasa ndani ya upinzani.

Ingawa viongozi wote wanakubaliana kuwa umoja ndio njia pekee ya kumng’oa Rais Ruto mwaka 2027, bado hawajakubaliana nani anafaa kuongoza tiketi hiyo.

Kwa mujibu wa wachambuzi, uchaguzi nchini Kenya hauamuliwi na umaarufu pekee.

Mchanganyiko wa maeneo, makabila, usimamizi wa miungano na hisia za ushirikishwaji huwa na uzito mkubwa sawa na umaarufu wa mgombeaji.

Kalonzo anaungwa mkono kwa hoja kwamba ana tajriba ya kisiasa ya miongo kadhaa, aliwahi kuwa Makamu wa Rais na amekuwa akisubiri nafasi ya kuwania urais kwa muda mrefu.

Kwa upande mwingine, Matiang’i anaonekana kuwa na taswira ya kiongozi mwenye uwezo wa kiutawala na anayekubalika na wapigakura wanaotaka mageuzi.

Naye Sifuna anaonekana kuwa sura mpya inayovutia zaidi vijana na Wakenya wanaotaka kizazi kipya cha uongozi.

Kura ya maoni ya Infotrak ilionyesha kuwa tiketi ya Kalonzo-Sifuna ndiyo inayopendelewa zaidi na wapigakura kwa asilimia 23.

Kwa upande mwingine, kura ya TIFA ilimpa Sifuna asilimia 15 ya uungwaji mkono kugombea urais, akifuatiwa na Matiang’i kwa asilimia 14 huku Kalonzo akipata asilimia 13.

Wachambuzi wanasema matokeo hayo yanaibua maswali magumu.

Iwapo Sifuna ndiye anayependwa zaidi, je, atakubali kuwa mgombea mwenza?

Na ikiwa Kalonzo ataacha tena azma baada ya kusubiri kwa miaka mingi, je, wafuasi wake watamuunga mkono mgombeaji mwingine?

Seneta wa Kitui Enoch Wambua amesema muungano wa upinzani na Linda Mwananchi utaendelea kushirikiana licha ya changamoto zozote.

“Makundi hayo mawili yana lengo moja; kuhakikisha Rais Ruto anahudumu muhula mmoja tu, na yatafanya kazi pamoja,” alisema.

Matiang’i pia amesisitiza kuwa mgombea wa urais anapaswa kupatikana kupitia mchakato wa wazi na unaokubalika na wote.

Kwa upande wake, msemaji wa muungano wa upinzani Dkt Mukhisa Kituyi amesema kuibuka kwa Linda Mwananchi kunamaanisha Sifuna sasa ni sehemu muhimu ya hesabu ya upinzani.

“Yupo mtoto mpya kwenye ulingo, Sifuna na timu yake. Lazima tuzungumze nao na tuone hatua wanazopanga kuchukua,” alisema.

Hata hivyo, changamoto nyingine kubwa ni eneo la Mlima Kenya.

Wachambuzi wanaonya kuwa kuacha eneo hilo nje ya tiketi ya urais kunaweza kupunguza ari ya wapigakura wake.

Ingawa Gachagua alitimuliwa afisini, wengi wanaamini bado ana ushawishi mkubwa wa kisiasa katika eneo hilo.

Wakili Nelson Osiemo anasema upinzani utapata wakati mgumu kuwashawishi wakazi wa Mlima Kenya kuunga mkono tiketi ambayo haina mmoja wao.

Kwa sasa, viongozi pekee kutoka eneo hilo waliotangaza nia ya kuwania urais ni kiongozi wa Safina Jimi Wanjigi na kiongozi wa People’s Liberation Party Martha Karua.

Kwa upande mwingine, Naibu Rais Kithure Kindiki ameendelea kuimarisha kampeni za Kenya Kwanza Mlima Kenya akisisitiza kuwa mustakabali wa eneo hilo uko ndani ya serikali ya Rais Ruto.

Sifuna amesema yuko tayari kushirikiana na Gachagua licha ya kuwa miongoni mwa maseneta waliopiga kura ya kumtimua afisini.

“Tutafanya kazi na yeyote anayeamini katika Katiba, utawala wa sheria na kwamba Rais Ruto hastahili kuongezewa hata siku moja madarakani,” alisema.

Viongozi wa upinzani wanasema bado hawajafikia uamuzi wa mwisho kuhusu mgombea wao wa urais na mgombea mwenza.

Wanatarajia kutangaza tiketi yao na mfumo wa kugawana madaraka kufikia Machi mwaka ujao.

Hadi wakati huo, mazungumzo yanatarajiwa kuendelea huku maslahi ya kikanda, kura za maoni na matarajio ya viongozi mbalimbali yakizidi kuathiri hesabu za kisiasa.