Habari

Oparanya sasa ndiye kigogo wa ODM aliyependekezwa kuwa mgombea mweza wa Ruto 2027

Na CECIL ODONGO August 3rd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WAZIRIwa Vyama vya Ushirika, Wycliffe Oparanya ameibuka chaguo bora ODM kwa wadhifa wa mgombea mwenza wa urais kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027, baada ya miezi kadhaa ya mashauriano na kampeni za ndani ya chama.

Hatua hiyo inajiri huku ODM ikijipanga kuingia katika mazungumzo na UDA kuhusu ushirikiano wa kisiasa.

Duru ndani ya chama zinaeleza kuwa viongozi wakuu wa ODM sasa wamekubaliana kumuunga mkono Bw Oparanya ili awe mgombea mwenza wa Rais Ruto.

Hali hiyo sasa inamweka kwenye kinyángányiro kikali dhidi ya Naibu Rais Profesa Kithure Kindiki, ambaye anapigiwa upato na viongozi wa UDA.

Awali Waziri wa Madini, Hassan Joho na Gavana wa Homa Bay, Gladys Wanga, walikuwa wakitajwa kama wanaoweza kuwa mgombeaji mwenza wa Rais Ruto lakini juhudi zao zinaonekana kufifia.

Bi Wanga sasa ameelekeza nguvu zake katika kampeni za kutetea kiti chake cha ugavana, huku Bw Joho akijikita katika kampeni za kuunga mkono azma ya Rais Ruto ya kuchaguliwa tena.

Uamuzi wa kumpendelea Bw Oparanya ulianza kujadiliwa Mei baada ya kukutana na kiongozi wa ODM Dkt Oburu Oginga pamoja na wabunge kadhaa wa Kakamega.

Kabla ya mkutano huo, Bw Oparanya alikuwa ametishia kukihama chama akidai eneo la Magharibi lilikuwa likitengwa katika uongozi na ugavi wa nafasi serikalini

Mbunge wa Khwisero, Christopher Aseka alisema mkutano huo ulisaidia kurejesha umoja kati ya viongozi wa Magharibi na uongozi wa chama.

“Wakati huo Oparanya alikuwa ametengwa na hali ndani ya chama haikuwa nzuri. Sasa tumemaliza tofauti zetu na wabunge wa ODM kutoka Magharibi tumeamua kumuunga mkono awe mgombea mwenza wa Rais Ruto. Tulihisi eneo letu lilikuwa limepuuzwa licha ya kuwa ngome muhimu ya marehemu Raila Odinga,” akasema Bw Aseka.

Mnamo Aprili 25, akiwa Kakamega, Bw Oparanya alisema viongozi wa Magharibi walipaswa kutambuliwa zaidi ndani ya ODM baada ya kifo cha Raila.

“Tumekuwa tukimuunga mkono Raila kwa dhati na lazima sasa tujue watu wa Magharibi watanufaika vipi ndani ya ODM. Tusipothaminiwa, tutalazimika kutafuta mwelekeo mwingine,” akasema Bw Oparanya.

Kwa mujibu wa Bw Aseka, mikutano kadhaa kati ya Bw Oparanya na Dkt Oburu imeimarisha nafasi yake ndani ya chama na kufufua ushawishi wa ODM Magharibi.

Baada ya kuibuka kama chaguo la ODM, chama kimempa Kiongozi wa Wachache katika Bunge la Kitaifa Junet Mohamed jukumu la kuongoza kampeni za kumuuza Bw Oparanya kote nchini.

Akizungumza Malava, Bw Mohamed alisema ikiwa UDA itatoa mgombea urais, basi ODM inapaswa kupewa nafasi ya mgombea mwenza.

“Uongozi una utaratibu wake na Oparanya ndiye anayefaa kuongoza Magharibi ndani ya ODM. Ikiwa UDA itatoa mgombea wa urais, basi ODM inastahili nafasi ya naibu rais, na hiyo inafaa kuendea Oparanya,” akasema.

Mbunge wa Butere, Tindi Mwale pia aliwataka wakazi wa Magharibi kumuunga mkono Bw Oparanya.

Duru pia zinaarifu kuwa Bw Oparanya alipata uungwaji mkono mkubwa katika mkutano wa Julai 2 ulioongozwa na Dkt Oburu na kuhudhuriwa na Mawaziri Hassan Joho, John Mbadi, Opiyo Wandayi, Bw Junet Mohamed na Mkurugenzi Mtendaji wa ODM Oduor Ong’wen.