Kimataifa

Mfichuzi wa sakata za ufisadi Sudan Kusini aachiliwa baada ya kuzuiliwa miezi miwili

Na REUTERS August 11th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

JUBA, Sudan Kusini:

MWANAHARAKATI kutoka Sudan Kusini aliyekuwa akifichua sakata za ufisadi na alitekwa Kenya mnamo Juni kabla ya kupelekwa Sudan Kusini, aliachiliwa baada ya kuzuiliwa kwa karibu miezi miwili, familia yake ilisema Jumatatu.

Athorbey Al-Gaddhaffy-Dit alirejea Nairobi Jumamosi na kwa sasa anapokea matibabu baada ya afya yake kuzorota alipokuwa kizuizini katika jiji kuu la Sudan Kusini, Juba, familia yake ilisema katika taarifa.

Gaddhaffy-Dit, ambaye pia ni raia wa Kenya, alikamatwa na wanaume waliokuwa wamejihami na kufunika nyuso zao baada ya kutoka katika kasino iliyoko viungani mwa Nairobi mapema Juni.

Mkewe aliripoti kutoweka kwake kwa polisi wakati huo, akitoa maelezo kutoka kwa mashahidi.

Mwanaharakati wa Kenya, Boniface Mwangi, alisema Juni kwamba Gaddhaffy-Dit alimweleza Aprili kuwa alikuwa ametoa taarifa kuhusu madai ya ufisadi wa kiwango cha juu kuhusu serikali ya Sudan Kusini.

Msemaji wa serikali ya Sudan Kusini Ateny Wek Ateny, hakujibu mara moja ombi la kutoa maoni kuhusu suala hilo.

Serikali ya Sudan Kusini imekuwa ikipuuza mara kwa mara madai ya ukiukaji wa haki za binadamu kwa utaratibu pamoja na ufisadi ulioenea nchini humo.

Maafisa wa Kenya na Sudan Kusini walisema Juni kuwa hawakuwa na taarifa kuhusu kutoweka kwa Al-Gaddhaffy-Dit.