Siasa

Changamoto za Linda Mwananchi kuhifadhi jina baada ya chama tofauti kupewa jina ‘LINDA’

Na JUSTUS OCHIENG August 12th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

HUENDA hakuna chama cha kisiasa nchini kinachofahamu umuhimu wa kulinda chapa yake kuliko Orange Democratic Movement (ODM).

Waanzilishi wake bado wanakumbuka jinsi kuchelewa kusajili jina la chama kulivyokaribia kuvuruga mipango yao kuelekea uchaguzi wa 2007.

Karibu miongo miwili baadaye, historia hiyo inaonekana kujirudia, safari hii ikihusisha mrengo uliotokana na ODM.

Kwa miezi kadhaa, Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna na washirika wake, akiwemo Gavana wa Siaya James Orengo na Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino, wamekuwa wakijenga vuguvugu la Linda Mwananchi kuwa chapa kubwa ya upinzani.

Hata hivyo, huku viongozi hao wakihamasisha wafuasi kote nchini, vita vingine vilikuwa vikiendelea kimyakimya katika Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Kisiasa (ORPP).

Hatimaye, Ofisi hiyo iliidhinisha usajili wa chama cha Liberty National Democratic Alliance (LINDA), hatua iliyozua mvutano kuhusu matumizi ya jina “Linda”.

Hali hiyo imewaweka viongozi wa Linda Mwananchi katika hali ngumu wanapojaribu kubadilisha vuguvugu hilo kuwa chama rasmi.

Kisa hicho kinafanana na masaibu yaliyowahi kukumba ODM.

Mwaka 2005, baada ya kampeni za kupinga Katiba iliyopendekezwa, viongozi wa upinzani walidhani jina hilo lingebadilika moja kwa moja kuwa chama.

Hata hivyo, wakili Mugambi Imanyara alikuwa tayari amechukua hatua na kuhifadhi jina Orange Democratic Movement.

Raila Odinga, William Ruto, Musalia Mudavadi, Kalonzo Musyoka na wenzao walipotaka kusajili chama hicho, waligundua jina lilikuwa tayari limechukuliwa.

Walilazimika kutumia jina ODM-Kenya, ambalo baadaye lilinaswa na mrengo wa Bw Musyoka.

Hatimaye, kikundi cha Raila na Ruto kililazimika kufanya mazungumzo na Bw Imanyara na kupata cheti cha awali cha ODM.

Tukio hilo likawa funzo muhimu kwamba katika siasa za Kenya, jina la chama ni muhimu kisiasa na kisheria.

Linda Mwananchi ilianza kama kampeni ya kupinga mrengo wa “Linda Ground” uliokuwa chini ya Kiongozi wa ODM, Dkt Oburu Oginga.

Baadaye ilikua na kuwa jukwaa la kitaifa, lenye ujumbe ulioratibiwa na mtandao wa wafuasi.

Wafuasi wake walisema walitaka kurejesha uwajibikaji ndani ya ODM na kuimarisha msimamo wa upinzani.

Hata hivyo, haikujulikana ikiwa viongozi wake walikuwa wamehifadhi kisheria jina hilo.

Mnamo Februari, Bw Charles Wanyonyi aliwasilisha ombi la kuhifadhi jina “Linda Mwananchi Party of Kenya”.

Mawakili wake wanasema Sheria ya Vyama vya Kisiasa inataka maombi yashughulikiwe kwa kuzingatia kanuni ya aliyetuma maombi kwanza.

Msajili alikataa ombi hilo, akisema jina hilo linafanana na majina mengine yaliyohifadhiwa.

Baadaye, baada ya mivutano ndani ya ODM kuongezeka, washirika wa Bw Sifuna waliwasilisha ombi la kuhifadhi jina Linda Mwananchi.

Wiki hii, ujumbe wao ulikutana na Msajili wa Vyama vya Kisiasa, Bw John Cox Lorionokou kutaka uamuzi wa awali upitiwe upya.

Hatua hiyo ilizua pingamizi kutoka kwa mawakili wa Bw Wanyonyi.

Walisema Msajili hawezi kufungua tena suala ambalo tayari liliamuliwa bila kumjulisha mwombaji wa kwanza.

Wakili Chris Omore alisema mwenye jina la chama hupata zaidi ya chapa.

“Anapata uwezo wa kujadiliana wakati wa kuunda miungano, ushawishi kuhusu ufadhili wa kampeni na haki ya kuwakilisha chama kisiasa,” alisema.

Hata hivyo, alisema umaarufu wa jina pekee hauwezi kupatia mtu umiliki wake kisheria.

Mzozo huo umezidi kuwa mgumu baada ya LINDA Party kusajiliwa rasmi.

Pauline Njoroge, mshirika wa Bw Sifuna, anadai kuna mkono wa serikali katika mvutano huo.

Anahoji kwa nini chama kinachoitwa Liberty National Democratic Alliance kitumie ufupi LINDA badala ya LNDA.

“Linda yetu si kifupi. Ni neno la Kiswahili linalowakilisha vuguvugu letu,” alisema.

Bi Njoroge alisema wafuasi wa Linda Mwananchi hawatakubali kupoteza jina hilo.

Hata hivyo, wachambuzi wanaonya kuwa hata Linda Mwananchi ikisajiliwa, huenda ikakabiliwa na changamoto kuhusu kufanana kwa majina ya vyama.

Bw Geoffrey Mboya alisema viongozi wenye uzoefu kwa kawaida hushughulikia masuala ya kisheria kabla ya kuanza kampeni kubwa.

“Viongozi wake wamefanikiwa kujenga chapa inayotambulika kitaifa, lakini kupata umiliki wa kisheria wa jina hilo kunaonekana kuchelewa,” alisema.

Kinachofanya hali hiyo kuwa ya kejeli ni kwamba ODM yenyewe iliwahi kupitia changamoto kama hiyo.

Katika sherehe za miaka 20 ya ODM zilizofanyika Mombasa mwaka jana, mwenyekiti mwanzilishi, Bw Henry Kosgey, alisimulia jinsi chama hicho kilivyokaribia kuvurugika baada ya kugundua kuwa Bw Imanyara alikuwa tayari amesajili jina ODM.

Sasa, miaka 20 baadaye, mrengo mmoja wa ODM unaonekana kukumbana na funzo lilelile.

Kwa Linda Mwananchi, vita sasa si kuhusu nani aliyeanzisha kauli hiyo au nani anavutia umati mkubwa zaidi.

Ni kuhusu nani aliyefika kwanza kwenye meza ya Msajili.

Na historia ya siasa za Kenya inaonyesha kuwa mara nyingi, anayelinda karatasi kwanza ndiye anayelinda jina.