Habari

Kagwe asema nchi haitalemewa na njaa licha ya mabadiliko ya tabianchi

Na CECIL ODONGO August 17th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

SERIKALI inapanga mikakati ya kuwasaidia wakulima kukabiliana na athari za ukame huku kipindi kirefu cha kukosekana kwa mvua kikitishia uzalishaji wa mahindi katika baadhi ya maeneo nchini.
Waziri wa Kilimo, Mutahi Kagwe alisema serikali itawasaidia wakulima walioathiriwa na mabadiliko ya hali ya hewa na kuweka mikakati ya kuhakikisha usalama wa chakula nchini.
Bw Kagwe alisema hayo baada ya kutembelea na kutathmini hali ya kilimo katika kaunti za Eldoret, Nandi na Trans Nzoia, ambako alitambua athari za ukame kwa uzalishaji wa mahindi.
Aliwahakikishia Wakenya kuwa nchi haitakabiliwa na uhaba wa chakula licha ya changamoto zinazowakumba wakulima.
“Hatutaruhusu Wakenya kuteseka na kulemewa na njaa kutokana na hali ya hewa iliyopo sasa,” akasema.
Waziri huyo pia alionya dhidi ya biashara ya mbegu bandia akisema inazorotesha uzalishaji wa kilimo na kusababisha wakulima kupata hasara.
Alisema baadhi ya wakulima hugundua kuwa walinunua mbegu bandia miezi mitano hadi sita baada ya kupanda, wakati mimea yao inaposhindwa kustawi.
Aliagiza vyombo vya usalama kuongeza juhudi za kukabiliana na wafanyabiashara wa mbegu hizo na akawataka wabunge kuunga mkono sheria itakayofanya uuzaji wa mbegu bandia kuwa uhalifu wa kiuchumi.
Wakulima walishauriwa kununua mbegu zilizoidhinishwa kutoka taasisi zinazotambulika kama Kampuni ya Mbegu (KSC) na Kampuni inayohusika na Utafiti kuhusu Mbegu za Kisasa (KALRO).
Mkurugenzi Mkuu wa KSC Sammy Chepsiror alisema kuna akiba ya kutosha ya mbegu nchini. Alisema mavuno ya mahindi mwaka jana yalifikia karibu magunia milioni 70 ya kilo 90.