Harambee Starlets kumenyana na Senegal leo WAFCON
Harambee Starlets watarejea dimbani leo dhidi ya Senegal katika mechi yao ya pili ya Kundi A ya Kombe la Mataifa ya Afrika kwa Wanawake (WAFCON) kwenye Uwanja wa Olympic mjini Rabat kuanzia saa mbili usiku saa za Kenya.
Baadae katika uwanja wa Moulay El Hassan mjini Rabat, Morocco watavaan na mahasimu wao Algeria kuanzia saa tano usiku saa za Kenya.
Kenya na Senegal zinatafuta pointi zao za kwanza baada ya kupoteza mechi za ufunguzi. Starlets walinyoroshwa 4-0 na wenyeji Morocco huku Senegal wakilimwa 2-0 na Algeria.
Senegal wanaingia mechi hiyo wakiwa na nafasi kubwa zaidi wakishika nafasi ya 79 duniani katika viwango vya Shirikisho la Soka Duniani (FIFA), huku Kenya ikiwa nafasi ya 128.
Kocha wa Starlets Beldine Odemba anatarajiwa kufanya mabadiliko katika kikosi chake baada ya kipigo dhidi ya Morocco.
“Senegal ni timu ambayo inatumia nguvu nyingi, wanakimbia sana na wanatumia miili yao vizuri. Tunajua watakachokuja nacho na tuko tayari kukabiliana nao,” alisema Odemba jana akifanya mahojiano na nawahabari.
Aliongeza kuwa kikosi chake kimefanyiwa maandalizi ya kisaikolojia na kimejifunza kutokana na makosa ya mechi iliyopita.
“Tunapaswa kutumia nafasi tunazopata. Tulikuwa na nafasi mbili nzuri dhidi ya Morocco, lakini hatukuzitumia. Tukiboresha hilo, matokeo yatakuwa tofauti.”
Beki Enez Mango alisema wachezaji bado wana imani ya kupata ushindi.
“Hii ni mechi muhimu kwetu. Tumejifunza kutokana na mchezo wa kwanza na kila mmoja ana ari ya kupambana. Tunaamini tunaweza kushinda,” alisema Mango.
Kocha wa Senegal Mame Moussa Cissé pia ameitahadharisha timu yake dhidi ya kuidharau Kenya.
“Kama Kenya imefuzu kucheza WAFCON, basi ilistahili kuwa hapa. Wana ari ya kupambana na wana wachezaji wenye vipaji,” alisema Cissé.
Mshindi wa mechi hiyo atafufua matumaini ya kutinga robo fainali, huku atakayepoteza akijikuta katika hatari kubwa ya kuaga mashindano mapema.