Habari

Mkuu wa runinga ya Telemundo, mkuu wa Ujasusi Ecuador miongoni mwa 7 waliofariki ajali ya helikopta

Na DAVID MUCHUI August 20th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WATU saba walioangamia katika ajali ya helikopta Mlima Ololokwe, Samburu walijumuisha Mkenya, Waamerika watano na raia wa Ecuador.

Waliofariki wanajumuisha rubani Mkenya na mkurugenzi wa kampuni ya African Heli Adventures Josh Outram, pamoja na Mkuu wa Kitengo cha Ujasusi cha Ecuador Michele Sensi-Contugi na mkewe Stephany Hollihan Yeaza.

Maafisa wa usalama wakiwa eneo la mkasa wa helikopta Mlima Ololokwe, Samburu. Picha|David Muchui

Imetambuliwa pia kwamba rais na meneja wa vituo vya runinga vya Telemundo jimbo la Florida Jose Suarez alikuwa miongoni mwa wakuu wa kampuni kutoka Amerika waliopoteza maisha yao. Wengine ni Roger Duarte, Adam Hlavaty na Henry Parra.

Utambulisho wa waliofariki ulithibitishwa kupitia ripoti ya polisi huku vyombo vya habari vya Amerika vikinukuu Kitengo cha Serikali kama kilivyothibitisha majina.

Maafisa wa usalama wakiondoa miili kutoka eneo la ajali ya helikopta, Mlima Ololokwe, Samburu. Picha|David Muchui

Watalii hao walikuwa wamepaa kutoka Suiyan, katika hifadhi ya Loisaba, Laikipia, mpaka Mlima Ololokwe wakati helikopta hiyo ilipoanguka katika kilima chenye mawe makubwa.

Kamanda wa Polisi wa Kaunti ya Samburu David Nkoroi alisema kwamba chanzo cha ajali hiyo bado hakijatambuliwa.

Ripoti zinasema kwamba Outram alikuwa rubani aliye na ujuzi na tajriba kubwa na ambaye amepaisha ndege katika maeneo ya vilima kwa miaka kadha kama mdau wa utalii na kusaidia kushika doria za angani katika hifadhi za wanyamapori.

Katika mahojiano ya awali na Loisaba Collection, Outram alieleza jinsi alivyopenda urubani na kutalii maeneo ya kaskazini mwa Kenya.

“Kaskazini mwa Kenya kuna mandhari tofauti sana katika eneo dogo. Ninachokiona kila siku ni jambo ambalo ninaamini kila anayekuja Kenya anapaswa kuliona,” alisema.

Alisema helikopta huwapa watalii nafasi ya kufikia maeneo ya mbali na ambayo hayajaathiriwa na shughuli nyingi za binadamu kaskazini mwa Kenya.

Wakati huo huo, kifo cha Sensi-Contugi na mkewe kilithibitishwa na serikali ya Ecuador kupitia taarifa iliyochapishwa kwenye akaunti rasmi ya X ya Rais Daniel Noboa.

“Katika wakati huu wa majonzi makubwa, Serikali ya Kitaifa inatuma rambirambi zake za dhati kwa familia zao, wapendwa wao na marafiki wa karibu,” ilisema taarifa hiyo.

Vyombo vya habari vya Ecuador viliripoti kuwa Sensi-Contugi aliwahi kuwa Waziri wa Usalama wa Ndani kati ya Aprili na Agosti 2024, kabla ya kuteuliwa kuwa mkurugenzi wa Kituo cha Kitaifa cha Ujasusi (CNI).

Alitajwa pia kuwa mshirika wa karibu wa Rais Noboa.

Nchini Amerika, NBC 6 iliripoti kuwa kifo cha Suárez, 55, kilithibitishwa kupitia taarifa ya pamoja ya viongozi wa NBCU News Group na Telemundo.

“Tumepokea kwa huzuni kubwa habari kwamba José amefariki katika ajali ya helikopta nchini Kenya. José alikuwa mfanyakazi bora aliyejali sana aliofanya kazi nao, jamii walizohudumia na jukumu muhimu la vituo vyetu katika maisha ya watu,” viongozi hao walisema.

Familia ya Duarte, 39, pia ilithibitisha kifo chake na cha waathiriwa wengine.

“Familia za Duarte na Valls zimevunjika moyo na kuhuzunika kutokana na ajali hii mbaya ya helikopta nchini Kenya iliyowaua wapendwa wetu,” familia hiyo ilisema.

Helikopta hiyo inayomilikiwa na Lady Lori, kampuni ya kukodisha ndege, ilianguka ikijaribu kutua Mlima Ololokwe, eneo maarufu kwa watalii kutokana na mandhari yake na machweo ya kuvutia.