Ruto adai Uhuru amekataa handisheki licha ya juhudi zake za kutaka wapatanishwe
HAKUNA siri kwamba uhusiano kati ya Rais William Ruto na mtangulizi wake Uhuru Kenyatta umeharibika.
Lakini kiwango cha uhasama kati ya viongozi hao wawili, ambao wakati mmoja walionekana kuwa washirika wasioweza kutenganishwa, unaonekana katika juhudi za Rais Ruto za miaka minne zilizolenga kurejesha uhusiano wao.
Katika mahojiano ya kipekee na Taifa Jumapili katika Ikulu ya Nairobi Ijumaa, Agosti 21, Rais Ruto alifichua kwa mara ya kwanza kwa undani jinsi alivyoshindwa kumshawishi Bw Kenyatta kujitenga na siasa za vyama na kuchukua nafasi ya kiongozi mstaafu anayewaunganisha Wakenya.
Rais alisema aliwahi kumtembelea Bw Kenyatta nyumbani kwake Ichaweri, Gatundu, Kiambu, na pia ofisini kwake karibu na Ikulu, akimshawishi kusaidia kujenga maono mapya ya taifa.
“Nilienda kumuona Ichaweri na pia katika ofisi yake hapa jirani na nikamuomba kwamba, kama kiongozi wa zamani wa nchi, na wa pekee aliye hai sasa, tafadhali tusaidie kujenga maono mapya ya nchi,” alisema.
Lakini kwa mujibu wa Rais, Bw Kenyatta alichagua kuendelea kushiriki siasa za upinzani.
“Mtangulizi wangu alikuwa na nafasi ya kuwa kiongozi wa kitaifa, na kuwa mtu wa kuunganisha nchi yetu. Lakini alichagua kushuka na kuwa kiongozi wa upinzani,” alisema.
Uhusiano wa Ruto na Kenyatta uliwahi kuwa miongoni mwa ushirikiano wenye nguvu zaidi katika siasa za Kenya.
Wawili hao waligombea urais pamoja mwaka 2013 na 2017 chini ya chama cha Jubilee.
Ushirikiano huo ulijengwa baada ya ghasia za baada ya uchaguzi wa 2007/08 na mashtaka katika Mahakama ya Kimataifa kuhusu Uhalifu (ICC) yaliyowakabili viongozi kadhaa wa Kenya.
Lakini mambo yalibadilika katika muhula wa pili wa Bw Kenyatta.
Handisheki ya Machi 2018 kati ya Bw Kenyatta na aliyekuwa kiongozi wa ODM Raila Odinga yalimuacha Dkt Ruto ametengwa kisiasa.
Mvutano huo ulifikia kilele katika uchaguzi wa 2022 ambapo Bw Kenyatta alikataa kumuunga mkono aliyekuwa naibu wake na badala yake akamuunga mkono Bw Odinga.
Dkt Ruto alishinda uchaguzi huo.
Sasa, miaka minne baada ya kuingia Ikulu, majeraha ya zamani bado yanaonekana.
Bw Kenyatta bado ni mwenyekiti wa Baraza la Azimio, chombo kikuu cha kufanya maamuzi katika muungano huo, na pia anaongoza chama cha Jubilee.
Baada ya kifo cha Bw Odinga, amempa kiongozi wa Wiper Patriotic Front Kalonzo Musyoka jukumu la kuongoza Azimio na anaunga mkono aliyekuwa Waziri wa Usalama wa Ndani Fred Matiang’i katika juhudi za kumuondoa Dkt Ruto madarakani mwaka ujao.
Lakini Rais Ruto alisema alijaribu kuzuia mgawanyiko huo.
Alifichua kuwa wakati mmoja alizungumza na Bw Odinga kuhusu haja ya viongozi wakuu wa kisiasa kufanya kazi pamoja kujenga maono ya muda mrefu ya Kenya.
“Sasa sisi ni wazee. Sisi ni viongozi wa nchi hii. Kwa nini tusifanye kazi pamoja, tujenge maono makubwa ambayo tunaweza kuyakabidhi kwa kizazi kijacho cha viongozi?” Rais alikumbuka akimwambia Bw Odinga.
Kwa mujibu wake, Bw Odinga alikubaliana naye na wakapendekeza kumtafuta Bw Kenyatta.
Mnamo Desemba 9, 2024, Rais Ruto alisafiri hadi nyumbani kwa Bw Kenyatta Ichaweri kwa mkutano wa ana kwa ana uliolenga kufungua ukurasa mpya kati ya viongozi hao wawili.
Miezi kadhaa baadaye, Bw Kenyatta alirejea Ikulu mnamo Agosti 2025 na kufanya mazungumzo ya faragha na Rais, yakiwemo masuala ya amani nchini DRC.
Lakini juhudi hizo hazikubadilisha uhusiano wao kisiasa.
Dkt Ruto sasa anamlaumu mtangulizi wake kwa kuchagua kuunga upinzani badala ya kusaidia kujenga mwafaka wa kitaifa.
Uhasama huo umeenea pia katika mjadala wa uchumi.
Rais alidai Bw Kenyatta alitabiri kuwa serikali yake ingeanguka ndani ya miezi mitatu kutokana na hali mbaya ya uchumi aliyokuwa ameacha.
“Kenya ilikuwa inakabiliwa na uhaba wa fedha za kigeni, mfumuko mkubwa wa bei, mikopo ghali na hofu kuhusu uwezo wake wa kutimiza majukumu ya nje,” alisema.
Kwa mujibu wa Rais, Bw Kenyatta aliwaambia washirika wake wa Azimio kuwa serikali mpya haingeweza kudumu.
“Alijua kuhusu uwezekano wa kushindwa kulipa deni, alijua hali ya uchumi,” alisema. “Nina hakika ana tatizo kwamba… niliweza kuongoza nchi na hatukushindwa kulipa.”
Rais pia alilinganisha deni la umma lililoachwa na tawala zilizotangulia.
Alisema utawala wa Daniel arap Moi uliacha deni la takriban Sh630 bilioni mwaka 2002, Mwai Kibaki Sh1.8 trilioni, huku Bw Kenyatta akiacha deni la karibu Sh10.3 trilioni.
Kwa sasa, alisema, deni linakaribia Sh13 trilioni.
Hata hivyo, Rais alikiri kwamba miradi ya miundombinu ya utawala wa Bw Kenyatta haikuwa mibaya.
“Utawala wa Uhuru haukuwekeza katika mambo yasiyofaa,” alisema.
Tofauti, kwa mujibu wa Dkt Ruto, ni kwamba serikali yake inatafuta njia mbadala za kufadhili miradi bila kutegemea sana mikopo ya serikali.