Habari za Kitaifa

Serikali yakataa wito wa Upinzani kuita ICC kwa suala la mashambulizi ya wahuni

Na LUKE ANAMI, JUSTUS OCHIENG August 24th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

SERIKALI imekataa wito wa upinzani na mashirika ya kiraia kwa Mahakama ya Kimataifa kuhusu Uhalifu (ICC) kuchunguza kuongezeka kwa ghasia za kisiasa nchini kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2027.

Serikali imesisitiza kuwa idara za usalama na taasisi za sheria nchini zina uwezo wa kukabiliana na vitisho hivyo.

Msimamo huo unajiri Amerika ikiongeza kampeni yake dhidi ya ICC, huku Muungano wa Ulaya na washirika wengine wa kimataifa wakitetea mahakama hiyo kama chombo huru cha haki duniani.

Mjadala huo umeibua kumbukumbu za ghasia za baada ya uchaguzi wa 2007, ambapo ICC ilianzisha uchunguzi kuhusu madai ya uhalifu dhidi ya binadamu kufuatia uchaguzi wa urais uliokumbwa na utata.

Mkuu wa Mawaziri na Waziri wa Masuala ya Nje na Wakenya wanaoishi ng’ambo, Musalia Mudavadi, alisema Kenya imejitolea kuzingatia utawala wa sheria na haina haja ya kupeleka uchunguzi wa uhalifu wa ndani kwa taasisi za kimataifa.

“Tuna wajibu wa kuimarisha na kulinda taasisi kama ICC,” alisema Bw Mudavadi katika mahojiano.

Alisema Kenya haijawahi kukataa kuheshimu utawala wa sheria, iwe katika uwanja wa kimataifa au ndani ya nchi.

“Serikali hii imefikishwa katika mahakama za humu nchini mara nyingi. Hatujawahi kukaidi maamuzi ya mahakama; daima tumeyaheshimu,” alisema.

Bw Mudavadi alikataa wito wa taasisi za kimataifa kuingilia kati, akisema mahakama za Kenya na idara za usalama zina uwezo wa kukabiliana na ghasia na uvunjaji wa sheria kuelekea uchaguzi wa 2027.

Alikumbusha Rais William Ruto alivyowahi kufikishwa ICC kuhusu tuhuma za ghasia za baada ya uchaguzi wa 2007.

“Rais wetu wa sasa, Ruto, alikuwa na ujasiri wa kukabiliana na ICC. Hii inaonyesha kwamba, mwishowe, anaheshimu utawala wa sheria,” alisema.

Kesi dhidi ya Rais Ruto iliondolewa baadaye kutokana na ukosefu wa ushahidi wa kutosha. Kwa jumla, Wakenya sita waliwahi kushtakiwa katika ICC, akiwemo Rais mstaafu Uhuru Kenyatta. Kesi zote zilitibuka.

Msimamo wa serikali unatofautiana na ule wa viongozi wa upinzani na mashirika ya kiraia yanayotaka uchunguzi wa kimataifa kuhusu kile wanachosema ni dalili za kuandaliwa kwa ghasia za kisiasa.

Mnamo Jumatano, Muungano wa Upinzani, muungano usio rasmi wa wakosoaji wa Rais Ruto, uliitaka Ofisi ya Mwendesha Mashtaka wa ICC kuanza kuchunguza matukio ya hivi majuzi ya ghasia za kisiasa nchini.

Kiongozi wa People’s Liberation Party Martha Karua, aliyesoma taarifa hiyo kwa niaba ya muungano huo, alitaja mashambulizi yaliyolenga aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua Rongai, Nakuru; tukio lililomlenga aliyekuwa Waziri wa Usalama wa Ndani Fred Matiang’i Mulot, Bomet; ghasia zilizokumba mkutano wa Linda Mwananchi Homa Bay; na makabiliano ya awali Keumbu, Kisii.

“Huu ni wito wa kuchukua hatua kuhusu ghasia za uchaguzi nchini Kenya,” alisema Bi Karua.

“Matukio ya ghasia za kisiasa yanayoongezeka katika maeneo mbalimbali ya Kenya hayawezi tena kupuuzwa kama makabiliano ya kawaida kati ya wafuasi wa kisiasa wanaopingana.”