Habari za Kaunti

Gavana asihi wakazi wa Taita Taveta wasiunge Gachagua

Na WINNIE ATIENO August 25th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

VIONGOZI wa Taita-Taveta wakiongozwa na Gavana Andrew Mwadime wamewaonya wakazi wa Pwani dhidi ya kuunga mkono siasa za upinzani zinazoongozwa na kinara wa chama cha DCP, Bw Rigathi Gachagua.

Bw Mwadime alisema Bw Gachagua hafai kupata uungwaji mkono kutoka eneo la Pwani kwa sababu hakufanya lolote la maana kwa eneo hilo alipokuwa Naibu wa Rais baada ya uchaguzi mkuu wa 2022.

Alisema Bw Gachagua amekuwa akiwaita Wapwani binamu zake lakini alipokuwa mamlakani hakuwasaidia.

“Tutakuwa sawa kweli kushirikiana na mtu ambaye alipokuwa uongozini alisema hatuna hisa kwa serikali ya Kenya Kwanza baada ya uchaguzi mkuu wa 2022? Tuongee na wananchi waingie kwa mkondo wa Kenya Kwanza. Tutafunga njia za upinzani, tutazunguka nyumba baada ya nyumba kuuza sera ya Rais,” alisema.

Badala yake, aliwasihi wakazi kumuunga mkono Rais William Ruto na kumpigia kura kwa asilimia 100 katika uchaguzi wa 2027, akisema serikali yake imewekeza katika miradi mbalimbali ya maendeleo katika eneo hilo.

“Lakini wataita na wataveta mko na shida gani jamani? Tuache nongo nongo nyingi, tumuunge mkono Rais Ruto kwa muhula wa pili. Tumepokea maendeleo mengi kutoka kwa Rais Ruto kwa muhula wa kwanza tu. Wengine wamekuwa marais na hakuna maendeleo waliyotuletea,” alisema Bw Mwadime akimpigia debe Rais Ruto.

Senet awa Taita Taveta Bw Jonnes Mwaruma, Mbunge wa Taveta Bw John Bwire, mwakilishi wa wanawake Bi Lydia Haika, aliyekuwa gavana wa Taita Taveta Bw John Mruttu waliapa kushirikiana na chama cha ODM kumtafutia kura Rais katika kaunti hiyo.

“Tujitume kumtafutia Rais Ruto kura sababu ametuletea maendeleo hasa katika sekta ya uchukuzi. Waambie wapinzani kuwa Rais ametuletea miradi ya maendeleo ya kihistoria,” alisema Bw Mruttu.

Bw Mwaruma alisema wapinzani wa Bw Ruto hawataki serikali ipeleke maendeleo sehemu zote nchini.

“Wanataka serikali iendelee na ubaguzi wa jadi wa miradi ya maendeleo. Rais ameleta usawa, haijalishi unatoka kabila ndogo au kubwa maendeleo yanaenda sambamba. Wale waliokuwa miaka iliyopita walitunyima maendeleo na haki yetu ndio maana lazima tumuunge mkono, hakuna tena kucheza siasa za pata potea,” alisema Bw Mwaruma.

Alisema atatembea kila kijiji kumtafutia kura Rais.

Hata hivyo walimtaka Rais Ruto kusimama imara na kupuuza wapinzani wake ambao, alisema, wamekuwa wakimkosoa na kumchafua kisiasa.

“Hata mwembe wenye maembe ndio hupigwa mawe. Utaendelea kupakwa matope kwa sababu unafanya kazi. Usipopakwa matope, inaonyesha hufanyi kazi. Kwa hivyo usijali, wewe endelea kuwafanyia Wakenya kazi,” alisema Gavana huyo.

Pia aliwasihi viongozi wa kaunti hiyo kushirikiana katika kumtafutia Rais Ruto kura kutoka nyumba hadi nyumba kuelekea uchaguzi wa 2027.

Alitaja ujenzi wa barabara na ukarabati wa reli ya zamani ya Voi-Taveta miongoni mwa miradi ambayo amesema imekuwa ikitekelezwa na serikali ya Rais Ruto katika eneo hilo.