MAONI: Kiti cha Mwakilishi wa Kike kimeongeza sauti ya wanawake bungeni?
NAFASI ya Mwakilishi wa Wanawake katika Bunge la Kitaifa iliundwa kuongeza sauti za wanawake katika chombo cha kutunga sheria.
Lakini nafasi hii inapokuwa kiti cha kudumu cha mwanasiasa mmoja, tunapaswa kujiuliza ikiwa bado inatimiza dhima yake pana.
Mwanamke anapopewa nafasi ya kuingia Bungeni kupitia kaunti, anapata uzoefu, mwonekano na mtaji wa kisiasa.
Kwa nini asitumie jukwaa hilo kuwavisha wengine viatu na kuingia katika ushindani wa kawaida wa ubunge?
Hapa ndipo uamuzi wa Esther Muthoni Passaris wa kutetea tena kiti cha Nairobi unapozua mjadala.
Passaris alikuwa amedokeza nia ya kuwania ubunge wa Makadara. Lakini sasa anaonekana kurudi kwenye kiti anachokalia.
Hakuna kosa la kisheria kwa yeye kufanya hivyo. Lakini kisiasa, jambo hili linahitaji kutafakariwa.
Millie Odhiambo, Martha Wangari na Beatrice Elachi kwa mfano walitumia nafasi za uwakilishi wa wanawake kama jukwaa la kujijenga, kabla ya kuhamia katika maeneo bunge ya kawaida.
Walipoondoka, nafasi hiyo iliweza kumpa mwanamke mwingine fursa ya kuingia Bungeni.
Tatizo si Passaris pekee. Tatizo ni mfumo wa fikra. Ikiwa kila Mbunge wa Kike wa Kaunti ataona nafasi hiyo kama kiti cha kutetea milele, nafasi hiyo itageuka kuwa mwisho wa safari badala ya kuwa daraja.
Usawa wa kijinsia hautafikiwa kwa kuhesabu wanawake wale wale kila baada ya uchaguzi. Utahitaji wanawake wapya kuingia, kukua kisiasa na kuchukua nafasi katika maeneo bunge ya kawaida.
- Mwandishi ni msomi na mtafiti wa taaluma za Kiswahili