DCI yachunguza picha iliyomsawiri Machele kama mhudumu harusini
WAPELELEZI mjini Mombasa wanachunguza kisa cha picha ya Mbunge wa Mvita, Mohamed Machele, kubadilishwa na kuonyesha kana kwamba alikuwa mhudumu katika harusi ambako alikuwa mgeni mkuu, katika kile kinachodaiwa kuwa njama ya kumwaibisha.
Idara ya Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI) imewasilisha ombi mahakamani ikitaka kupewa ruhusa ya kuchunguza simu ya mkononi inayohusishwa na aliyekuwa mshirika wa karibu wa mbunge huyo, Bw Haani Omar Swaleh, huku uchunguzi wa madai ya unyanyasaji wa mtandaoni ukiendelea.
Bw Machele alihudhuria harusi ya mwana wa Kamanda wa Polisi wa Kanda ya Pwani, Ali Nuno, mnamo Juni 20 katika eneo la Nyali, Mombasa, ambako alipigwa picha kadhaa akiwa pamoja na wageni wengine.
Kwa mujibu wa stakabadhi za mahakama, mbunge huyo alishtuka baadaye alipojulishwa kuwa picha yake ilikuwa ikisambaa kwa wingi mitandaoni.
Picha hiyo ilikuwa imehaririwa na kuonyesha kana kwamba alikuwa amevalia mavazi ya mhudumu katika harusi hiyo na kuchapishwa kwenye majukwaa mbalimbali ya mitandao ya kijamii, ikiwemo WhatsApp ya Bw Swaleh.
“Baada ya kuhudhuria hafla hiyo, aliarifiwa kwamba alikuwa akivuma mtandaoni. Picha yake akiwa amevalishwa mavazi yaliyomwonyesha kama mhudumu katika harusi hiyo ilikuwa imechapishwa kwenye akaunti mbalimbali za mitandao ya kijamii, ikiwemo WhatsApp ya mshukiwa,” stakabadhi hizo zilisema.
Akiwa amekerwa na picha hiyo, Bw Machele aliripoti tukio hilo katika Kituo Kikuu cha Polisi Mombasa, chini ya nambari ya OB 49/23/7/ 2026.
Inspekta Joseph Ngatia, mpelelezi wa DCI, alisema mbunge huyo aliripoti tukio hilo miongoni mwa sababu nyingine kwa kuwa yeye ni mtu mashuhuri na mbunge anayehudumu.
Jumanne, DCI iliwasilisha ombi mahakamani ikimtaja Bw Swaleh kama mshukiwa anayechunguzwa kuhusu picha hiyo iliyohaririwa.
Wapelelezi wanasema Bw Swaleh alikamatwa Agosti 20 na simu aina ya iPhone 11 ikachukuliwa kutoka kwake.
Simu hiyo ina nambari mbili za IMEI na, kwa mujibu wa stakabadhi za mahakama, inaaminika kuwa ndiyo iliyotumika kubadilisha picha hiyo.
Orodha ya vitu vilivyopatikana iliandaliwa baada ya simu hiyo kuchukuliwa.
DCI inataka idara ya Uchunguzi wa Kisayansi cha Kitengo cha Polisi cha Kupambana na Ugaidi (ATPU) kipewe ruhusa ya kuishikilia simu hiyo, kuifikia na kuifanyia uchunguzi pamoja na kutoa taarifa kutoka kwa akaunti za WhatsApp, Facebook na TikTok kwa kipindi cha Juni 20 hadi Julai 20, 2026.
Inspekta Ngatia alisema uchunguzi huo wa kisayansi utawasaidia wapelelezi kubaini mazingira ya picha hiyo na kupata ushahidi utakaotumika mahakamani.
Wapelelezi pia wanataka mahakama iagize kitengo hicho cha ATPU kuandaa ripoti kuhusu taarifa zilizotolewa kwenye simu hiyo na kutoa cheti cha ushahidi wa kielektroniki kwa mujibu wa Kifungu cha 106B (4) cha Sheria ya Ushahidi.
Inspekta Ngatia alisema taarifa wanazotaka kupata ni za kibinafsi na zinaweza kufikiwa tu kwa idhini ya mahakama.
“Ni kupitia amri hii pekee ambapo ATPU inaweza kufikia, kuchunguza kwa njia ya kisayansi na kutoa taarifa hizo za kibinafsi zilizohifadhiwa kwenye simu ya mshukiwa,” alisema.
Aliongeza kuwa taarifa zitakazopatikana zitawasaidia wapelelezi kukusanya na kuthibitisha ushahidi unaohusiana na malalamishi hayo.
Uchunguzi huo unahusu madai ya unyanyasaji wa mtandaoni unaotokana na kuundwa, kuhaririwa na kusambazwa kwa picha ya mbunge huyo kwenye mitandao ya kijamii.
Kosa hilo linachunguzwa chini ya Kifungu cha 27 cha Sheria ya Matumizi Mabaya ya Kompyuta na Uhalifu wa Mtandaoni ya mwaka 2018.
Wapelelezi wanataka kubaini jinsi picha hiyo ilivyohaririwa, aliyehusika katika kuisambaza na iwapo vitendo hivyo vinaweza kuainishwa kama kosa chini ya sheria hiyo.