Maoni

MAONI: Ushindani wa kisiasa usiwe wa kuvunja nchi wala kuibua uhasama

Na BENSON MATHEKA August 27th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MJADALA kuhusu amani na uwajibikaji wa viongozi unapaswa kupewa uzito unaostahili uchaguzi mkuu wa 2027 unapokaribia.

Hivyo basi, Uzinduzi wa Mwongozo kuhusu Uchaguzi Usio na Vurugu wa 2027 uliotayarishwa na Tume ya Kitaifa ya Uwiano na Utengamano (NCIC) umejiri kwa wakati muafaka, ambapo dalili za kutovumiliana kisiasa, matamshi ya chuki na taarifa za kupotosha zinaanza kujitokeza.

Historia ya Kenya imeonyesha kwamba uchaguzi ni nguzo muhimu ya demokrasia, lakini pia unaweza kuwa chanzo cha migawanyiko iwapo hautasimamiwa kwa busara na uwajibikaji.

Kwa sababu hiyo, wito wa NCIC kwamba ushindani wa kisiasa usije ukawa kwa gharama ya maisha ya wananchi, umoja wa taifa au utulivu wa nchi unapaswa kuungwa mkono na kila Mkenya.

Ni jambo la kutia moyo kwamba, mwongozo huu haijawekwa kama jukumu la taasisi moja pekee.

Badala yake, unahimiza ushirikiano kati ya serikali za kitaifa na kaunti, idara za usalama, vyama vya siasa, mashirika ya kiraia, viongozi wa dini, vyombo vya habari, vijana na wadau wa maendeleo.

Mtazamo huu wa pamoja unatambua ukweli kwamba, amani na mshikamano haviwezi kujengwa na kundi moja peke yake.

Msingi wa uchaguzi wa amani hujengwa kabla ya siku ya kupiga kura.

Hujengwa kupitia lugha ya heshima, kuimarishwa kwa taasisi za umma, kushughulikiwa kwa malalamiko ya raia na kukuza mahusiano mazuri kati ya jamii mbalimbali.

Kauli za viongozi zina nguvu kubwa katika kuunganisha au kugawanya wananchi.

Ndio maana viongozi wa kisiasa, wanaowania nyadhifa na watu wote wenye ushawishi wanapaswa kujizuia, kuonyesha uzalendo na uwajibikaji katika matamshi yao.

Vilevile, suala la vijana linastahili kuangaliwa kwa jicho pevu.

NCIC imeeleza wazi kwamba vijana hawapaswi kuonekana kama nyenzo za kutekeleza vurugu za kisiasa, bali washirika wa kujenga amani.

Huu ni ujumbe muhimu kwa jamii na kwa viongozi wa kisiasa ambao mara nyingi wamekuwa wakitumia nguvu na hamasa ya vijana kwa malengo yanayohatarisha utulivu wa nchi.

Mapambano dhidi ya matamshi ya chuki, ukabila na kupotosha pia yanahitaji kupewa kipaumbele.

Katika enzi ya mitandao ya kijamii, ujumbe unaochochea uhasama unaweza kusambaa kwa haraka na kuathiri maelfu.

Ni wajibu wa kila mwananchi kupima taarifa kabla ya kuzisambaza na kukataa kushiriki katika kampeni zinazolenga kugawanya taifa.

Kenya ina nafasi ya kuonyesha ukomavu wa kidemokrasia na nguvu ya mshikamano wake wa kitaifa.

Uchaguzi wa 2027 unapaswa kuwa mfano wa ushindani wa kisiasa unaoheshimu tofauti za maoni bila kuzigeuza kuwa sababu za uhasama.

  • Matheka ni mhariri wa habari