Dimba

Zogo latokota majagina wa riadha wakitaka makaburi karibu na uga wa Keino yabomolewe

Na TITUS OMINDE August 28th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MVUTANO mkali unaohusu upanuzi wa uwanja wa mamilioni ya pesa wa Kipchoge Keino umechukua mkondo mpya baada ya kundi la wanariadha mashuhuri waliostaafu North Rift wakitaka ubomozi wa makaburi uendelee.

Wanariadha hao wakiongozwa na mwanariadha mkongwe Abraham Chelang’a wanataka utawala wa kaunti ya Uasin Gishu kuendelea na mpango wa kubomoa makaburi ya kihistoria ya Wakristo ambayo yamekuwa kando ya uwanja huo kwa zaidi ya karne moja.

Pendekezo la kubomoa makaburi kwa upanuzi wa kisasa ili kuwa na sehemu ya kufanyia mazoezi ya kujiandaa, limeibua mjadala mkali wa umma; huku familia za watu waliozikwa hapo na makundi ya kuhifadhi urithi wa eneo hilo yakipinga vikali pendekezo hilo.

Hata hivyo, wanariadha wa zamani wanahoji kuwa mji wa Eldoret—ambao kwa muda mrefu umekuwa ukijulikana kama makao makuu ya riadha duniani—unahitaji sana miundombinu ya michezo ya viwango vya kimataifa, na kwamba hoja za kihisia hazipaswi kukwamisha maendeleo ya kisasa ya michezo.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini Eldoret siku ya Alhamisi, Bw Chelang’a alisisitiza msimamo wake wa kutaka makaburi husika yabomolewe, akisema kuwa thamani ya kiuchumi kutokana na michezo katika uwanja wa viwango vya kimataifa ni kubwa zaidi kuliko kuhifadhi eneo hilo la zamani la makaburi.

“Hatuwezi kuruhusu historia kuzuia mustakabali wa vijana wetu. Thamani ya uwanja wa kisasa wa hadhi ya kimataifa kwa eneo hili ni kubwa zaidi kuliko kuhifadhi makaburi yenye umri wa zaidi ya karne moja. Makaburi haya yapo mahali ambapo uwanja unapaswa kupanuliwa kama eneo la kufanyia mazoezi ya kujianda kushiriki mashindano. Bila uwanja huo wa mazoezi, Shirikisho la Riadha Duniani (World Athletics) halitaidhinisha uwanja huo kwa ajili ya mashindano ya kimatiafa,” alisema Bw Chelang’a.

Bw Chelang’a alitoa wito kwa serikali ya kaunti kusimama imara licha ya kuongezeka kwa shinikizo za kusitisha upanuzi lengwa.

Alihimiza utawala wa kaunti, chini ya uongozi wa gavana Jonathan Bii, kupuuza vitisho kutoka kwa wale wanaopinga mradi huo na kuendelea na upanuzi.

Ujenzi wa uwanja huo unapaswa kukamilika kabla ya mwezi Oktoba kwa ajili ya maandalizi ya sherehe za kitaifa za mashujaa mnamo Oktoba 20.