Kuria ‘atabiri’ kuhusu atakayeapishwa kuwa rais 2027
ALIYEKUWA Waziri Moses Kuria ameibua mjadala kuhusu uchaguzi wa urais wa 2027 baada ya kutoa kauli tata kuhusu atakayeapishwa kuwa rais baada ya uchaguzi huo.
Kuria, ambaye ni kiongozi wa Chama Cha Kazi (CCK), aliandika kwenye mitandao ya kijamii Jumatano usiku, Agosti 26, 2026, akionekana kudokeza kuwa tayari anajua kitakachotokea katika uchaguzi huo.
“2027: Sijui nani atashinda. Lakini najua nani ataapishwa,” Kuria aliandika.
Katika kauli hiyo fupi hakutaja jina la mtu anayetarajia ataapishwa kuwa rais, hali iliyowaacha wafuasi wake wakikisia maana aliyokusudia.
Kuria ameendelea kumuunga mkono Rais William Ruto hata baada ya kuondoka serikalini.
Tangu ajiuzulu kama mshauri wa Rais Ruto, Kuria amerejea kikamilifu katika siasa akitoa maoni kuhusu masuala ya kisiasa.
Alitoa kauli hiyo siku ambayo aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua alitoa madai kuhusu maandalizi ya uchaguzi wa 2027.
Gachagua, ambaye sasa anaongoza chama cha upinzani cha DCP, alishutumu utawala wa Rais Ruto na IEBC kwa kuweka mazingira ya kuvuruga uchaguzi wa 2027.
Gachagua alielekeza wasiwasi wake hasa kwenye ununuzi wa teknolojia ya uchaguzi, akidai mchakato huo unaweza kutumiwa kuathiri matokeo ya uchaguzi.
Pia alimuonya Mwenyekiti wa IEBC Erastus Ethekon kusimama na Wakenya, akisema jaribio lolote la kuvuruga uchaguzi litakuwa na madhara makubwa.
Aidha, alidai kushindwa kwa Ruto 2027 kutakuwa kwa kishindo kiasi kwamba hakutaweza kufichwa kupitia kuvuruga mchakato wa uchaguzi.
Hata hivyo, madai hayo yamepuuzwa na maafisa wakuu wa serikali.
Katika hali hiyo, kauli tata ya Kuria imeongeza mwelekeo mpya katika mjadala wa kisiasa unaozidi kushika kasi kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.