Siasa

Sifuna apanda bei, ang’ang’aniwa na mabalozi na vinara wa Upinzani

Na MWANDISHI WETU September 11th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

SENETA wa Nairobi, Edwin Sifuna, anaendelea kuimarika kisiasa kitaifa huku akivutia viongozi wa upinzani na wanadiplomasia wa kimataifa, jambo linaloashiria kuongezeka kwa ushawishi wake katika siasa za Kenya kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka ujao.

Katika siku za hivi majuzi, ofisi ya Sifuna imekuwa kitovu cha mikutano muhimu ya kisiasa na kidiplomasia.

Miongoni mwa waliomtembelea ni Balozi wa Ufaransa nchini Kenya, Arnaud Suquet, pamoja na Kaimu Balozi wa Australia nchini Kenya, Andrew Barnes, waliokutana naye katika nyakati tofauti.

Sifuna alisema Balozi Suquet alimtembelea kumuaga kabla ya kumaliza kipindi chake cha huduma nchini Kenya. Katika ujumbe wake, Seneta huyo alimtaja mwanadiplomasia huyo kama rafiki yake.

Siku moja kabla ya hapo, Sifuna alikuwa mwenyeji wa Barnes na ujumbe wake katika ofisi yake jijini Nairobi.

Seneta huyo alisema walijadili masuala mbalimbali ya maslahi ya pamoja, huku ziara hiyo ikiongeza uzito wa hadhi yake inayoongezeka kimataifa.

Mikutano ya kidiplomasia imekuwa sehemu muhimu ya kuongezeka kwa hadhi ya kisiasa ya Sifuna.

Amewahi kukutana na Balozi wa Amerika nchini Kenya, Marc Dillard, katika Ubalozi jijini Nairobi, ambapo walijadili ushirikiano wa muda mrefu kati ya Kenya na Amerika pamoja na mikakati ya kuimarisha uhusiano wa kiuchumi kati ya mataifa hayo mawili.

Katika taarifa baada ya kikao hicho, Dillard alisema walijadili namna ya kujenga uchumi imara wa ubunifu unaowanufaisha wananchi wa nchi zote mbili.

Agosti 27, 2026, Sifuna alikutana na Balozi wa Uingereza nchini Kenya Matt Baugh, katika makazi ya mwanadiplomasia huyo jijini Nairobi.

Mkutano huo ulifanyika wakati Seneta huyo anaendelea kuimarisha vuguvugu la Linda Mwananchi na kupanua mtandao wake wa kisiasa kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka ujao.

Mikutano hiyo ya kidiplomasia inafanyika wakati Sifuna anapitia mabadiliko makubwa ya kisiasa.

Mwanzoni mwa mwaka, alikuwa Katibu Mkuu wa chama cha ODM, moja ya vyama vikuu vya upinzani nchini.

Hata hivyo, kuondolewa kwake katika wadhifa huo mnamo Juni kumemjenga kama kiongozi wa kitaifa anayevuka mipaka ya chama chake cha zamani.

Ingawa kuondolewa kwake kulionekana kama pigo kisiasa, wachambuzi wengi wanaamini hatua hiyo imempa uhuru wa kujijenga nje ya mfumo wa chama.

Badala ya kutetea maamuzi ya taasisi ya ODM, sasa ameonekana kuwa sauti ya kundi la viongozi wanaotaka upinzani uwe huru na mkali zaidi dhidi ya serikali.

Katika miezi ya hivi majuzi, Sifuna amejenga vuguvugu la Linda Mwananchi, linalohimiza uwajibikaji serikalini na kulinda maslahi ya wananchi.

Kupitia vuguvugu hilo, amefanya ziara katika maeneo mbalimbali ya nchi, ambapo amekuwa akihutubia mikutano mikubwa ya umma na kujenga mtandao wake wa kisiasa.

Umaarufu wake unaonekana kuongezeka hata miongoni mwa wafuasi wa ODM.

Tafiti za maoni zimeonyesha kuwa, sehemu kubwa ya wanachama wa chama hicho wanaunga mkono msimamo wake wa kuendeleza upinzani huru badala ya kushirikiana na serikali kupitia mpango wa serikali jumuishi.

Kadri umaarufu wake unavyoongezeka, ndivyo viongozi wakuu wa upinzani pia wameanza kujihusisha naye kwa karibu zaidi.

Jana, Sifuna aliongoza ujumbe wa Linda Mwananchi katika mkutano na aliyekuwa Waziri wa Usalama wa Ndani na mgombea urais wa Jubilee, Fred Matiang’i.

Mkutano huo ulihudhuriwa pia na Gavana wa Siaya James Orengo, Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi, Seneta wa Kisii Richard Onyonka na Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino.

Akizungumza baada ya kikao hicho, Osotsi alisema viongozi hao walijadili namna ya kuimarisha vuguvugu la “Wantam” pamoja na kueneza ushirikiano ndani ya upinzani mpana wa kitaifa.

Kwa mujibu wa Osotsi, mazungumzo hayo ni sehemu ya juhudi za kuwaleta pamoja viongozi wanaotaka mabadiliko ya kisiasa nchini.

Alisisitiza kuwa mashauriano hayo yataendelea kuwahusisha viongozi wengine wa upinzani katika siku zijazo.

Kabla ya kukutana na Matiang’i, Sifuna pia alikuwa amefanya mazungumzo na kiongozi wa chama cha Wiper, Kalonzo Musyoka, nyumbani kwake Karen.

Kundi la Linda Mwananchi lilisema viongozi hao walijadili umuhimu wa kushirikiana katika kulinda demokrasia ya kikatiba na kuimarisha misingi ya taifa.

Sifuna amekuwa akisisitiza haja ya viongozi wa upinzani kuungana ili kukabili serikali ya Rais Ruto.

Amesema ni lazima viongozi hao washirikiane kulinda katiba na kuhakikisha sauti za wananchi hazipuuzwi.

Hii ni mara ya pili katika kipindi cha miezi miwili kwa Sifuna na Kalonzo kukutana.

Ushirikiano huo unaongeza hisia kuwa viongozi wa upinzani wanapanga mikakati ya pamoja kuelekea uchaguzi mkuu ujao.

Wachambuzi wa siasa wanaamini kuwa kinachomtofautisha Sifuna na viongozi wengine wa upinzani ni uwezo wake wa kuvutia kizazi kipya cha wapiga kura.

Akiwa mmoja wa viongozi vijana zaidi katika siasa za kitaifa, amejijengea taswira ya mwanasiasa anayewakilisha mabadiliko ya kizazi ncha Gen Z na siasa mpya zinazolenga uwajibikaji.

Kwa mujibu wa mchambuzi wa siasa na mwanasheria Thomas Maosa, ongezeko la mikutano kati ya Sifuna na wanadiplomasia wa mataifa yenye ushawishi mkubwa duniani linaonyesha kwamba kiongozi huyo sasa anatambulika zaidi ya mipaka ya ODM na siasa za eneo la Nairobi.

“Mabalozi hukutana na viongozi wengi, lakini wanapomtafuta mwanasiasa mara kwa mara, inaonyesha kuwa wameanza kumwona kama sauti muhimu katika mazungumzo ya kitaifa. Sifuna ameanza kujijenga kama sura inayoweza kuathiri mwelekeo wa siasa za upinzani na hata siasa za Kenya kwa ujumla,” alisema Maosa.