• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 9:35 PM
MKASA WA ETHIOPIA: Ruto, Mudavadi na Maraga watuma risala za rambirambi

MKASA WA ETHIOPIA: Ruto, Mudavadi na Maraga watuma risala za rambirambi

Na PETER MBURU

VIONGOZI mbalimbali Jumatatu waliendelea kutuma jumbe za rambirambi kwa familia za watu walioangamia katika mkasa wa ajali ya ndege iliyokuwa ikisafiri kutoka Ethiopia kuelekea Jijini Nairobi, Kenya, wote wakieleza kuwa vifo hivyo vya watu 157 ni pigo kwa dunia.

Baada ya ajali hiyo ambayo iliacha familia nyingi kwa huzuni, viongozi hao wakiongozwa na Rais Uhuru Kenyatta na kiongozi wa chama cha ODM Raila Odinga walitumia mitandao ya kijamii kufariji familia hizo, na kuziombea amani.

“Wakenya wenzangu ambao wamepoteza wapendwa wao katika mkasa mbaya wa ajali ya ndege #ET302, Mungu awape nguvu ya kukabiliana na hali hii ngumu. Tunaelewa uchungu mnaopitia na tuko nanyi katika maombi,” akasema Bw Odinga, kupitia mtandao wa Twitter Jumatatu.

Jaji Mkuu David Maraga aidha alijiunga na viongozi waliokuwa wakiomboleza na familia hizo, akisema ajali hiyo ni mkasa wa kuhofisha.

“Najiunga na Wakenya na ulimwengu mzima kuomboleza walioangamia katika ajali ya ndege iliyokuwa ikitoka Ethiopia. Mawazo yangu yako kwa familia na washirika wa wale wote waliopoteza maisha yao. Mungu awape amani na nguvu ya kukabili hali hii,” akasema Bw Maraga.

Naibu Rais William Ruto Jumapili jioni naye alisema “Nimehuzunishwa na habari kuhusu ajali ya ndege iliyokuwa ikitoka Ethiopia kuelekea Nairobi asubuhi ya leo, mawazo yetu na maombi yako kwa familia za wale wapendwa wao walikuwa wakisafiri katika ndege hiyo.”

Rais Kenyatta pia Jumapili alisema “Tumehuzunishwa na habari kuhusu ajali ya ndege iliyokuwa ikitoka Ethiopia ambayo iliripotiwa kuanguka dakika sita baada ya kupaa, ikielekea Kenya. Maombi yangu yanaelekezwa kwa familia na washirika wa wale waliokuwamo.”

Kiongozi wa chama cha ANC Musalia Mudavadi aidha aliomboleza pamoja na waliopoteza wapendwa, kama viongozi wake walivyotuma jumbe, pia naye akitumia mtandao wa Twitter kutuma rambirambi zake.

You can share this post!

Ashangaza kujificha msituni miaka 10 kuhepa ukorofi wa mkewe

Ushindi kwa Thika Queens na Trans Nzoia Falcons

adminleo