• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
Serikali ikome kuwabagua wabunge wanawake wa NASA – Passaris

Serikali ikome kuwabagua wabunge wanawake wa NASA – Passaris

Na CHARLES WASONGA

HUKU ulimwengu ukiadhimisha Siku ya Kimataifa ya Wanawake Alhamisi, wabunge wa kike wa upinzani wameilaumu serikali kwa kuibagua katika masuala yanayowahusu wanawake.

Mbunge Mwakilishi wa Wanawake wa Nairobi Bi Esther Passaris Jumatano alidai serikali imewanyima wabunge wa NASA kibali cha kushiriki katika Kongamano la pili la Tume kuhusu hadhi ya Wanawake (CSW2) linaloanza wiki ijayo jijini New York, Amerika.

“Sio haki kwa serikali kutoa kibali kwa wabunge wa kike wa Jubilee pekee na kuwanyima wenzao wa NASA ambao pia waliteuliwa kusafiri kwa kongamano hilo linaloanza tarehe 12 mwezi huu. Wabunge wanawake hawafai kugawanywa kwa misingi ya kisiasa hasa ikiwa wanaenda kuwakilisha nchi,” akasema Bi Passaris.

Alitoa malalamishi hayo katika hoteli moja jijini Nairobi baada ya kuongozwa uzinduzi wa ripoti kuhusu changamoto zilizowakabiliwa wanawake walioshiriki katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2017.  Ripoti hiyo kwa jina “The Journey of Women Candidates in the 2017 General Elections” ni zao la uchunguzi uliofadhiliwa na shirika la ActionAid Kenya.

Hata hivyo, Mwenyekiti wa Muungano wa Wabunge Wanawake (KEWOPA) Purity Ngirichi alikana madai hayo akisema hana habari kwamba baadhi ya wenzake hawajapata kibali cha kushiriki katika kongamano hilo.

“Ujumbe wa Kenya, haswa sisi kama wanachama wa KEWOPA, haijapokea habari kama hizo. Hata hivyo, nitawasiliana na Wizara ya Mashauri ya Kigeni kwa maelezo zaidi,” akasema Mbunge huyo wa Mwakilishi wa Kaunti ya Kirinyaga.

Baadhi ya masuala yatayojadiliwa katika kongamano hilo ni changamoto na mafanikio katika mchakato mzima wa kuwapiga jeki wanawake na wasichana wa mashambani kiuchumi, kijamii na kisiasa.

Jumatano, Bi Passaris alitoa wito kwa wanawake kujitokeza kwa wingi kupigania viti vya kisiasa katika chaguzi zijazo ili waweze kupata nafasi ya kubuni sera ya maongozi ya kuchochea maendeleo nchini.

“Inasikitisha kuwa katika uchaguzi mkuu uliopita ni asilimia tisa pekee ya wanawake walishinda viti. Hii ni sawa na wanawache 157 pekee, idadi ambayo haitoshi kubisa ikizingatiwa kuwa asilimia 52 ya Wakenya ni wanawake. Kwa hivyo, nawahimiza wanawake kujitokeza kwa wingi kutafuta viti vya uongozi,” akasema Mbunge huyo wa chama cha ODM.

You can share this post!

Serikali inabagua wabunge wanawake wa NASA – Passaris

Mzozo wa kilabu cha Simmers: Mmiliki ataka wakurugenzi...

adminleo