• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 8:55 AM
Wiper yasema Raila alisaliti NASA kukutana na Rais Kenyatta

Wiper yasema Raila alisaliti NASA kukutana na Rais Kenyatta

Katibu Mkuu wa chama cha Wiper, Bw Peter Mathuki

Na BENSON MATHEKA

CHAMA cha Wiper sasa kinasema kiongozi wa ODM Raila Odinga aliwasaliti vinara wenzake kwa kukutana na Rais Uhuru Kenyatta bila kuwafahamisha.

Katibu Mkuu wa chama hicho Peter Mathuki alisema kulingana na Wiper mkutano huo haukuwa wa NASA.

“Tangazieni watu kwa haraka sana kwamba vyama tanzu vya NASA, hasa sisi Wiper hatukuhusishwa katika mkutano wa jana. Huu ni usaliti”, Bw Mathuki aliambia Taifa Leo kwa simu.

Alisema kiongozi wa chama cha Wiper Kalonzo Musyoka ambaye ni kinara mwenza wa NASA hakufahamu kuhusu mkutano wa Ijumaa.

“Tulishangaa kufahamu kuhusu mkutano huo. Tunashangaa watu wakidai hatuna msimamo ilhali Wakenya wanaweza kujionea ni nani ndiye watermelon,” alisema Bw Mathuki.

Alieleza kwamba Bw Musyoka alikuwa nchini mkutano huo ulipofanyika. “Kiongozi wetu alikuwa na angali nchini. Sababu za kutofahamishwa kuhusu mkutano huo ni ishara haukuwa wa NASA,” alisema.

Bw Mathuki alipuuzilia mbali uwezekano wa mkutano kuandaliwa kwa dharura akisema Bw Odinga alisoma taarifa iliyoandikwa.

“Taarifa hiyo ilikuwa imetayarishwa na kiongozi wa hadhi ya Bw Odinga na hawezi kupapia taarifa ambayo hana uhakika nayo,” alisema Bw Mathuki.

You can share this post!

TUKO PAMOJA: Uhuru na Raila walikutana baada ya mashauriano...

Mbunge atahadharisha kuhusu mkutano wa Uhuru na Raila

adminleo