• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 2:08 PM
Kioja mwizi wa pikipiki kuirejesha huku akilia

Kioja mwizi wa pikipiki kuirejesha huku akilia

Na CORNELIUS MUTISYA

KAVIANI, MACHAKOS

KIOJA kilishuhudiwa sokoni hapa, jamaa aliyeiba pikipiki alipoirejesha kwa mwenyewe huku akilia kutokana na masaibu chungu nzima yaliyomwandama.

Kulingana na mdokezi, mwenye pikipiki hiyo aliiegesha nje ya duka moja mwendo wa saa tatu usiku na kuingia ndani kununua bidhaa. “Polo alijitoma dukani kununua bidhaa na kuacha pikipiki nje ya duka ilivyokuwa desturi yake,’’ alisema mdokezi.

Inasemekana alipotoka nje hakuipata pikipiki yake.

Inadaiwa kwamba, polo aliye mcha Mungu alimwendea pasta mmoja maarufu ili amuombee aweze kuipata pikipiki yake aliyotegemea kujitafutia riziki.

“Mtumishi wa Mungu aliomba na kumuahidi polo kuwa angeipata pikipiki yake baada ya siku tatu,’’ alisema mdaku wetu.

Twaarifiwa kwamba polo alirejea kwake akiwa na matumaini kuwa ‘miujiza’ ingetendeka. Siku tatu zilipotimu, alishangaa alipomuona jamaa mmoja akisukuma pikipiki yake huku akiangua kilio kama mtoto mchanga!’

“Ukistaajabu ya Musa, utaona ya Firauni. Mwizi wa pikipiki alimrejeshea mwenyewe huku akilia,’’ alisema mdokezi.

Penyenye za mtaa zaarifu kuwa, umati ulifika mahali hapo kushuhudia kioja hicho huku wengi wao wakitisha kumtia kiberiti mwizi huyo ili awe funzo kwa wengine wenye tabia kama hiyo.

Hata hivyo, mwenye pikipiki aliwakataza kuchukua sheria mikononi mwao.

Alipohojiwa, mwizi alisema kwamba tangu aibe pikipiki hiyo, familia yake ilikumbwa na mfululizo wa nuksi.

Aliomba radhi na akasamehewa. Alionywa dhidi ya kujihusisha na visa vya wizi na akaenda zake huku akilia kwa simanzi na huzuni nyingi.

“Polo alikiri kwamba alitafuta huduma za pasta mmoja maarufu baada ya kuibiwa pikipiki yake,’’ alisema mdokezi.

WAZO BONZO…

You can share this post!

Kidosho pabaya kupapasa polo mbele ya majirani

KIFO CHA NASA: Dalili zote za muungano kusambaratika

adminleo