• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
Tumetoka mbali pamoja, Ruto amkumbusha Uhuru

Tumetoka mbali pamoja, Ruto amkumbusha Uhuru

 FLORAH KOECH na WYCLIFF KIPSANG

NAIBU Rais William Ruto ameendelea kumkumbusha Rais Uhuru Kenyatta jinsi wametoka mbali tangu 2013, na kueleza matumaini yake kuwa chama cha Jubilee hakitasambaratika, kwani walikianzisha kama mbinu ya kuunganisha Wakenya.

Dkt Ruto aliwakosoa viongozi wa Jubilee ambao wamekuwa wakilalamika kuhusu mambo ya chama hicho wazi, akiwaambia waache kujiaibisha na badala yake wasuluhishe tofauti zao ndani ya chama.

Akizungumza alipokuwa eneo la Eldama Ravine, Kaunti ya Baringo, Dkt Ruto aliwahakikishia wakazi kuwa chama hicho kiko imara, licha ya malumbano ambayo yamekuwa yakishuhudiwa kwa miezi sasa, na madai ya majuzi kuwa kuna mpango wa kumuua.

Alisema hayo wakati wafuasi wake waliendelea kumshinikiza Rais avunje baraza la mawaziri, kwa madai kuwa limegawanyika.

“Tuliamua na Rais kuunda chama baada ya kugundua kuwa siasa za Kenya zilikuwa zimezingirwa na chuki, ubinafsi na ukabila. Kulingana nami, hilo bado halijabadilika na sijafurahia,” akasema Dkt Ruto.

“Tulipounda chama hiki, tulilenga kubadili siasa za nchi hii. Tulitaka kumaliza siasa za migawanyiko, chuki na fujo, ili tuwaunganishe Wakenya bila kujali makabila yao ama mirengo ya kisiasa wanakotoka,” akaongeza Naibu Rais.

Alisema sababu ya baadhi ya viongozi katika chama hicho kulalamika kuwa kimegawanyika ni kwa kuwa hawaelewi kwanini kiliundwa.

Lakini aliwataka kuacha kulalamika katika vyombo vya habari, na badala yake wakalalamike katika chama.

“Jubilee haiko kwa ajili ya uchaguzi ambao umepita ama ambao unakuja. Ina kazi bora zaidi ya siasa na chaguzi. Kupeleka malalamishi na propaganda kwa vyombo vya habari badala ya chama ni usaliti,” akasema.

Aidha, aliendelea kujitetea kuhusu michango yake makanisani ambayo amekuwa akiingiliwa, akisema anawekeza mbinguni.

“Tuna jukumu la kujenga kanisa kulingana na Biblia. Mungu anasema tuwekeze mali zetu mbinguni na hivyo ndivyo tunafanya. Wengine wanaoamua kuwekeza katika mambo mengine huo ni uamuzi wao,” akasema Dkt Ruto.

Naibu Rais alikuwa ameandamana na Waziri wa Maji Simon Chelugui, katibu katika idara ya unyunyiziaji maji Fred Segor, kiongozi wa wengi Seneti Kipchumba Murkomen na Gavana wa Baringo Stanley Kiptis. Wengine ni mbunge wa Eldama Ravine Moses Lessonet, wa Mogotio Daniel Tuitoek, wa Baringo Kaskazini William Cheptumo na wa Nakuru mjini Mashariki David Gikaria.

Lakini wakati akisema hayo, wandani wake walikuwa wakimtia presha Rais kuwa avunje baraza la mawaziri, na kuzungumza kuhusu madai ya njama ya kumuua.

“Wakenya walitarajia kuwa Rais angewatimua mawaziri waliotajwa katika madai ya njama hiyo huku uchunguzi ukiendelea,” Gavana wa Nandi Stephen Sang akasema.

Wakati huo huo, wabunge Oscar Sudi (Kapseret) na Didmus Barasa (Kiminini) walitishia kuanika kanda ya video ya mkutano ambapo mpango wa kumuua Dkt Ruto uliandaliwa, ikiwa Idara ya Upelelezi(DCI) haitakamilisha uchunguzi huo na kusema kilichoendelea kwa wiki moja.

“Kukamatwa kwa Dennis Itumbi (Mkurugenzi wa mawasiliano ya kidijitali Ikulu) ilikuwa hatua ya kuwahadaa Wakenya tu. Tunataka kuarifiwa kilichofanyika katika hiyo mikutano,” akasema Bw Sudi.

You can share this post!

Madaktari Makueni waweka historia

WAKILISHA: Mshairi chipukizi ajongea jukwaani

adminleo