• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
UKUMBI WA LUGHA NA FASIHI: Nafasi ya Kiswahili katika ujenzi wa jamii mpya ya Afrika

UKUMBI WA LUGHA NA FASIHI: Nafasi ya Kiswahili katika ujenzi wa jamii mpya ya Afrika

Na CHRIS ADUNGO

LUGHA ni chombo muhimu sana cha mawasiliano kilichoundwa na sauti za nasibu za kusemwa na kutumiwa na jamii ya utamaduni fulani.

Jinsi ambavyo zipo jamii nyingi za tamaduni mbalimbali duniani, vivyo hivyo ziko lugha mbalimbali zilizoundwa kukidhi haja ya mawasiliano ya tamaduni mbalimbali.

Maingiliano ya jamii zenye tamaduni na lugha mbalimbali yanayotokana na mashirikiano katika shughuli za biashara na nyinginezo za kijamii, huzusha haja ya kuwepo kwa lugha moja itakayoweza kuwaunganisha watu hao wenye tamaduni na lugha mbalimbali.

Maingiliano kama hayo yanaweza kuwa katika viwango mbalimbali.

Kiwango cha kwanza ni kile cha mtu binafsi; ambapo mtu hutoka kwenye jamii yake na kwenda kuishi kwenye jamii inayozungumza lugha tofauti na ile ya kwao.

Katika hali kama hiyo, mtu huyo itabidi ajifunze lugha ya jamii ile ya pili ili aweze kuwasiliana nao.

Kiwango cha pili ni kile kinachohusisha mkusanyiko wa watu waliotoka kwenye tamaduni mbalimbali na hawana hata lugha moja ya kuwaunganisha. Watu kama hawa wakikaa pamoja, huweza kuzusha lugha ya kati ambayo katika

hatua za mwanzo itajulikana kama pijini na baadaye kama krioli.

Kiwango cha tatu ni kile ambacho maingiliano ya watu wenye tamaduni na lugha mbalimbali husababisha kuteuliwa kwa lugha moja miongoni mwa lugha zao na kutumika kama chombo cha mawasiliano na cha kuziunganisha jamii zote husika.

Kiwango hiki chaweza kujitokeza katika ngazi ya wilaya, mkoa, nchi, kanda, bara na hata ulimwengu mzima.

Ukoloni

Wakati wa enzi ya ukoloni katika Afrika Mashariki, haja ya kuwepo kwa lugha moja itakayotumika hususan katika elimu katika nchi zote za makoloni ya Mwingereza wakati ule, yaani Tanganyika, Kenya, Uganda ilijitokeza.

Matokeo ya haja hii ni kuchaguliwa kwa Kiswahili, hususan lahaja ya Kiunguja itumike kama lugha ya kufundishia shuleni.

Urasmi

Vilevile, matokeo ya haja hiyo yalikuwa ni kuundwa kwa Kamati ya Lugha ya Afrika Mashariki mnamo mwaka 1925 na kuanza kazi mnamo 1930 iliyopewa mamlaka ya kuisanifisha lugha ya Kiswahili, ili kuwe na namna moja rasmi ya kusema na kuandika katika Afrika Mashariki.

Baada ya nchi za Afrika Mashariki kupata Uhuru, haja ya kuwepo kwa lugha moja kwa kila nchi kwa ajili ya mawasiliano na wananchi, na katika shughuli mbalimbali za kiserikali na za kijamii ikajitokeza.

Tanganyika ilipojipatia uhuru mwaka 1961 (Tanzania tangu 1964) ikajichagulia Kiswahili kilichokuwa kimekwishaenea nchi nzima kiwe Lugha ya Taifa na Kiingereza kiwe Lugha Rasmi katika masuala ya kiserikali na kimataifa.

Kenya ilipopata uhuru mnamo 1963, kwa kuwa haikuwa na lugha iliyokuwa imeenea nchi nzima, na kwa kuhofia mivutano ya kuchagua lugha moja ya wenyeji, haikuteua lugha ya taifa.

Hata hivyo, Kiingereza kiliteuliwa kuwa Lugha Rasmi katika masuala ya kitaifa na kimataifa. Kiswahili ambacho kilikwishaanza kuongelewa na watu wengi, kilitumika katika kuwasiliana na wananchi katika mikutano ya siasa, biashara nk.

Uganda ilipata uhuru mwaka 1962. Ijapokuwa katika kipindi hicho lugha ya Luganda ilikuwa imekwishaenezwa nchini na watawala wa Kiganda, si Luganda wala lugha nyingine yoyote ya wenyeji iliyopteuliwa kuwa Lugha ya Taifa.

Whitely (1969), anadai kuwa “uteuzi wa watawala kutoka Buganda kutawala sehemu mbalimbali za Uganda, kulichangia kueneza lugha, lakini watawala hawa walionekana kama walikuwa wanapanua utawala wa Buganda, hivyo mwishowe lugha yao na wao wenyewe walichukiwa”.

Lugha nyingine ambayo ilikuwa imeenea kwa kiasi fulani nchini ilikuwa Kiswahili.

Ijapokuwa pendekezo la Gavana Sir W.F Gowers la kukifanya Kiswahili kuwa lugha ya elimu na utawala na vilevile kuwa lugha ya mawasiliano (lingua franca) nchini kote lilipingwa vibaya na Kabaka Sir Daudi Chwa mnamo 1929, Kiswahili kiliendelea kupata mashiko.

Whitely (1969:70-71) anaripoti kuwa Kiswahili kiliendelea kutumiwa na polisi, sehemu za Kaskazini kuwasiliana na watu ambao hawajui Kiingereza na Luganda. Vilevile wanilotiki wa Uganda walitumia sana Kiswahili kuwasiliana na makabila mengine. Kiswahili kilitumika pia kwenye mipira, na sehemu nyingine ambazo lugha za Kiingereza na Luganda hazikuhitajika au hazikuwezekana kutumika.

Uteuzi

Hata hivyo, ili kukidhi haja ya mawasiliano, baada ya uhuru, Kiingereza kiliteuliwa kuwa Lugha Rasmi katika masuala ya kitaifa na kimataifa. Matumizi ya Kiswahili nchini Uganda yalishika kasi baada ya kuondolewa madarakani kwa Idd Amina Dada na kuingia madarakani kwa Rais Yoweri Kaguta Muzeveni, ambaye aliishi Tanzania kwa miaka kadhaa na elimu yake ya Chuo Kikuu kuipatia huko.

Katika bara la Afrika kwa ujumla, uundwaji wa ushirikiano wa kiuchumi miongoni mwa nchi huru, pamoja na mambo mengine, ulizingatia kigezo cha lugha ya mawasiliano. Kihistoria, ushirikiano baina ya Waafrika ulianza kabla nchi za Afrika hazijapata uhuru kati ya 1920-1957 chini ya dhana ya Upanafrika.

Lengo kuu lilikuwa kuzikomboa nchi hizo zitoke kwenye ut- awala wa kikoloni. Ushirikiano baina ya nchi huru za Kiafrika ulianza baada ya nchi za Afrika kuanza kupata uhuru kati ya mwaka wa 1957 na 1960.

Malengo makuu ya awali ya ushirikiano yalikuwa kwanza, ni kupigania uhuru wa makoloni yaliyobaki napili, kuunda muungano wa kisiasa wa bara zima chini ya serikali moja ya shirikisho.

Baada ya nchi nyingi za Kiafrika kujipatia uhuru kuanzia mwaka 1960, mgawanyiko ukaanza kujitokeza na wazo la kuwa na muungano wa kisiasa likaanza kufifia.

Badala ya kufikiria muungano wa nchi zote za Afrika, makundi mbalimbali yakaanza kujitokeza.

Kwa mfano, mwaka 1961, Ghana, Guinea, Egypt, Mali, Morocco, Libya na Algeria wakaunda kundi la Casablanca, makoloni yaliyobaki ya Wafaransa pamoja na Nigeria, Ethiopia, Liberia, na Siera Leone wakaunda kundi la Monrovia.

You can share this post!

Ligi yatarajiwa kuanza ila kombe la kuwaniwa halijanunuliwa

BONGO LA BIASHARA: Sura mpya ya uchoraji na jinsi vijana...

adminleo