• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 8:50 AM
MAWAIDHA YA KIISLAMU: Kumcha Mungu kuna faida nyingi kwa mwanadamu humu duniani

MAWAIDHA YA KIISLAMU: Kumcha Mungu kuna faida nyingi kwa mwanadamu humu duniani

Na HAWA ALI

MOLA wetu anapotuamrisha jambo jema basi lina maslaha kwetu sisi. Na anapotukataza jambo baya pia lina maslaha kwetu sisi.

Basi ikiwa ndivyo hivyo inamaanisha kuwa Mola wetu angelijua kama kuna jambo jingine kubwa zaidi na lenye kuleta faida au manufaa kwetu kuliko hili la “Kumcha Mungu” basi bila shaka asingetuficha bali angelituusia ili tupate kutekeleza na lituongoze katika njia Yake na kuokoka na adhabu Zake.

Mwenyezi Mungu S.W.T. kasema katika Surat Aali-`Imraan aya ya 102, Maana yake, “Na iogopeni siku ambayo mtarudishwa kwa Mwenyezi Mungu, kisha kila nafsi italipwa kwa ukamilifu yote iliyoyachuma; nao hawatadhulumiwa.”

Faida za kumcha Mungu

Faida za kumcha Mwenyezi Mungu S.W.T. ni nyingi kupita kiasi lakini kwa kurahisisha mambo hapa nitazitaja kwa uchache tu.

1)Mwenyezi Mungu amemuahidi mchaMungu kuwa hawezi kumtupa bali atamheshimu na kumjali kuliko watu wote wale wasiomcha Mungu. Kwa dalili ya Qurani, kasema katika Suratil Hujuraat aya ya 13, “

Maana yake, “…Hakika aheshimiwae sana miongoni mwenu mbele ya Mwenyezi Mungu ni yule amchaye Mungu zaidi katika nyinyi…”

2) Mola Subhaanahu Wataala humuokoa Mwislamu mcha Mungu katika kila balaa itakayompata hapa duniani na kumwepusha nayo mbali na balaa hiyo, wakati ambapo yeye mwenyewe atashangaa na pengine kwa ule mshangao wake asiweze kuamini vipi ameweza kuokoka nayo. Kwa hali hiyo uchaMungu ni kinga za balaa na uokovu kwake. Kama alivyotuhadithia Mwenyezi Mungu Subhaanahu Wataala katika Surat Talaaq aya ya 2,

Maana yake, “…Na anayemcha (anayemuogopa) Mwenyezi Mungu, (Allah) humtengenezea njia ya kuokoka (katika kila balaa).”

3)Mwenyezi Mungu Subhaanahu Wataala. humrahisishia mchaMungu mambo yake yote hapa duniani yamwendee na kuyaona mepesi kwake bila kuhangaika na kupata taabu yoyote ile. Kama alivyotufahamisha katika Surat Talaaq aya ya 4, “…Na anayemuogopa Mwenyezi Mungu, (Mola) humfanyia mambo yake kuwa mepesi.”

4) Mwenyezi Mungu Subhaanahu Wataala amewasifu na kuwapongeza wachaMungu kwa subira zao na khofu ya kumuogopa Mola wao, na mfano wa Kiswahili unasema “Mstahamilivu hula mbivu.” Kama alivyotuelezea katika Surat Aali-`Imraani aya ya 186,

Maana yake, “…Na ikiwa mtasubiri na mkamcha (Mwenyezi Mungu), basi haya ni katika mambo muhimu sana ya kufanywa (na watu).”

5) Mola Subhaanahu Wataala amewadhamini wote wale wachaMungu ikiwa wao watasubiri na kumcha Yeye tu, basi hila za adui au mchawi au hasidi yeyote yule hazitawadhuru. Kwani Mwenyezi Mungu anaona yote wanayoyatenda Binaadamu na Majini na Yeye Ndie Mwenye kuwahifadhi na kila aina ya balaa. Kama alivyotusimulia katika Surat Aali- `Imraani aya ya 120, Maana yake, “…Na ikiwa mtasubiri na mkamcha (Mwenyezi Mungu basi), hila zao (maadui) hazitakudhuruni.”

6) Mwenyezi Mungu Subhaanahu Wataala. anawatia moyo wale wachaMungu pamoja na wafanyao wema kwamba Yeye daima yupo nao, wasikate tamaa bali wazidi kumtegemea Yeye na atawanusuru na kuwasaidia kwa kila jambo au tatizo litakalowapata. Kama alivyowaahidi katika Suratin Nahl aya ya 128, Maana yake, “Kwa hakika Mwenyezi Mungu yu pamoja na wale wanaomcha, na wale wafanyao wema.”

7) Mola Subhaanahu Wataala. humsamehe mchaMungu madhambi yake na kumzidishia ujira wake siku ya Kiyama. Kama alivyomwambia katika Surat Talaaq aya ya 5, Maana yake, “…Na anayemcha Mwenyezi Mungu humfutia maovu (madhambi) yake na humpa ujira mkubwa.”

8) Allah Subhaanahu Wataala anawapa moyo wachaMungu kwamba Yeye anawapenda sana kuliko wengine kwa sababu ya vile vitendo vyao vizuri wanavyovifanya, na kwa kule kumheshimu Mola wao inavyotakiwa. Kama alivyotuelezea katika Surat Tawba aya ya 7,

Maana yake, “…Hakika Mwenyezi Mungu anawapenda wanaomcha (wanaomuogopa).”

9) Mwenyezi Mungu S.W.T. huwatumia wachaMungu Malaika Wake kwa kuwapa khabari njema wakati ule wa kufikwa na mauti kwamba wasiwe na khofu wala huzuni kwa kuiaga dunia na kuwaacha kama vile: Wake zao na mali yao na watoto wao na jirani zao; kwani Mola wao atawabadilishia kwa mambo mazuri zaidi kuliko hayo ikiwa pamoja na kuwaingiza katika Pepo Yake.

Kwa kauli ya Mwenyezi Mungu S.W.T. katika Surat Yuunus aya ya 63 na ya 64, “

Maana yake, “Wale ambao wameamini na wakawa wanamcha Mungu (wanafuata amri Zake na wanajiepusha na makatazo Yake). Wao wana mema katika maisha ya duniani na katika Akhera…”

You can share this post!

REDS MAVIZIONI: Liverpool wala tupa kukata Norwich EPL

Nyoro amnyorosha Baba Yao

adminleo