• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 9:50 AM
PAMBO: Msaidie mchumba wako kupiga deki upate asali bila kipimo

PAMBO: Msaidie mchumba wako kupiga deki upate asali bila kipimo

Na BENSON MATHEKA

Unapomsaidia kazi za nyumbani bila shaka unampunguzia uchovu hivyo kumuacha katika hali mzuri ya kukupatia burudani tosha
-Alfred Ombati, Shirika la Love Care, Nairobi

IKIWA wewe ni mwanamume mzembe unayependa kuketi kwenye kochi mkeo akifanya kazi za nyumbani, unajinyima uroda kutoka kwake.

Wataalamu wanasema kwamba wanaume wanaosaidiana kazi za nyumbani na wake zao hupata shibe la uroda na pia ni magwiji wa shughuli chumbani.

Utafiti huo ulifichua kwamba wanaume wanaochangia kazi za nyumbani hawakaushwi na wake zao wanapotaka uroda. Na sio kukaribishwa kushiriki tendo lenyewe pekee, hukolezwa uhondo wa ngoma mara kwa mara.

Kulingana na mtafiti Dkt Matt Johnson, wa chuo kikuu cha Alberta, Canada aliyeshiriki katika utafiti huo uliochukua miaka mitano, kiwango cha kazi za nyumbani ambacho mwanamume hufanya huchangia kiwango cha burudani anachopata kutoka kwa mkewe.

Utafiti huo ulishirikisha wanandoa 1,338 kutoka Ujerumani na ulilenga kubaini iwapo kiwango cha kazi za nyumbani wanachofanya wanaume kina uhusiano na maisha ya uroda ya wanandoa.

“Katika uhusiano wa kimapenzi kiwango cha kazi hutegemea majukumu ya wachumba wenyewe. Kuna wanaume wanaoweza kupangusa meza na kuchochea hisia za mapenzi za wachumba wao na kuna wanaopiga deki na kukosa kusisimua watu wao,” aeleza Bw Johnson.

Hata hivyo Alfred Ombati wa shirika la Love Care jijini Nairobi anasisitiza kwamba mchango wa wanaume katika majukumu ya nyumbani huongeza joto la mahaba.

“Unapomsaidia mke au mchumba wako kwa kazi za nyumbani bila shaka unampunguzia uchovu. Kwa hivyo, mnapoingia chumbani atakuwa katika hali mzuri ya kukupatia burudani,” aeleza Bw Ombati.

Mwenzake wa shirika la Big Hearts Hellen Wanjiku anasema wanaume hujinyima uroda kwa kuwaachia wanawake kazi zote za nyumbani.

 

Asiwe mtumwa

“Unapomchukua mchumba wako kama mtumwa kwa kumuachia kazi za nyumbani huku ukitulia kochini na kutazama runinga, haufai kutarajia burudani faraghani,” aeleza.

Utafiti wa Johnson ulibaini kwamba wanawake wakihisi kuwa wachumba wao hawawachukulii kama watumwa, huwa wanawafungulia milango ya tendo la ndoa mara kwa mara na kuwa na maisha ya uroda ya kuridhisha.

Alisema matokeo ya utafiti huo ni muhimu kwa wanandoa wanaotaka kudumisha joto katika maisha yao ya uroda.

Bi Wanjiku asema wanandoa wanaposaidiana na kushirikiana katika majukumu ya nyumbani, mili yao hutulia na kuwa katika nafasi nzuri ya kulishana uroda.

“Ni suala la kisaikolojia na rahisi sana ambalo watu huwa wanapuuza na kwa kufanya hivyo wanaangamiza maisha yao ya tendo la ndoa,” asema na kukiri kwamba kuna vizingiti vya kitamaduni ambavyo watu wanafaa kuepuka iwapo wanataka kuboresha maisha yao ya uroda.

Utafiti huo unasema kwamba baadhi ya watu huwa wanaepuka kazi za nyumbani wakidhani kufanya hivyo kutawasaidia kuwa na maisha bora ya tendo la ndoa.

 

Kukaushwa

“Wanaofanya hivyo hujipata wameharibu uhusiano wao na wachumba wao na kukaushwa wanapohitaji burudani. Na hata wakipatiwa burudani huwa sio katika hali ya kuridhisha, wanapimiwa kama dozi,” aeleza Bw Ombati.

Anashauri watu kujukumika kwa kila hali iwapo wanataka kufurahia maisha ya uroda na wachumba wao. “Usipojukumika, usitarajie mchumba wako akukoleze mapenzi.

Mbali na kutekeleza majukumu yako kama kiongozi wa familia, msaidie mke wako kulea watoto, kupika, kupiga deki, kufua nguo na kupeleka watoto shuleni. Ukifanya hivi, tarajia mabadiliko makubwa katika maisha yenu ya burudani faraghani,” asema.

Utafiti mwingine wa Sharon Sassler mwanasaikolojia wa chuo kikuu cha Cornell, New York, unafichua kwamba kiwango cha uroda miongoni mwa wanandoa kote ulimwenguni kinaendelea kushuka, isipokuwa wale wanaogawana majukumu ya nyumbani kama kupika na kupiga deki.

“Siku hizi kujenga mapenzi ni mchango wa kila mtu. Ni wanaogawana majukumu ambao wanaendelea kufurahia tendo la ndoa kwa kiwango cha juu kinachowaridhisha,” aeleza.

 

You can share this post!

Matiang’i, Kihalangwa na Boinnet waitwa kortini...

‘Si lazima ukate miti ndipo uchome makaa’

adminleo