• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 12:58 PM
Wakili Mutinda aponea kusukumwa jela kwa kuwa ‘mwongo’

Wakili Mutinda aponea kusukumwa jela kwa kuwa ‘mwongo’

Na RICHARD MUNGUTI

WAKILI wa Serikali Charles Mutinda yuko na bahati kama mtende kwa vile aliponyoka kusukumwa jela kwa madai hakuwaarifu Waziri wa Usalama Fred Matiang’I, Inspekta Jenerali wa Polisi (IG) Joseph Boinnet na Mkurugenzi wa Idara ya Uhamiaji Meja mstaafu Gordon Kihalangwa wamfikishe wakili mbishi Miguna Miguna makamani Alhamisi.

Mawakili Cliff Ombeta, John Khaminwa , Harun Ndubi na James Orengo waliomba Jaji George Odunga amsukume Mutinda jela kwa kukaidi agizo la korti kwa “kutowakabidhi agizo la korti wafike kortini wakiandamana na Dkt Miguna.”

“Huyu wakili wa Serikali anadanganya. Ni mdanganyifu. Alikaidi agizo la hii korti kwamba Miguna afikishwe kortini leo,” alisema Khaminwa.

Dkt Khaminwa alisema Mutinda hakuchukulia suala hilo kwa makini ndipo washtakiwa hawakufika kortini. “Naomba uamuru Mutinda asiwahi kuhudumu kama wakili na kwamba asithubutu kufika mbele ya mahakama yoyote kwa vile amekaidi sheria kama wakuu hao wa serikali waliokwepa mahakama.”

Bw Ombeta alisema Mutinda ni “mwongo na hata hafai kusimama kortini bali anatakiwa kufukuzwa aende nyumbani.”

Ombeta alishangaa jinsi Bw Mutinda hakuwaona Matiang’i, Kihalangwa na Boinnet ilhali waliapa afidaviti aliyotumia kukata rufaa na kesi nyingine ya kuomba maagizo ya Jaji Roselyn Aburili yatupiliwe mbali. “Huyu wakili Mutinda ni mdanganyifu.”

Bw Orengo alisema Bw Mutinda anapasa kupewa adhabu moja na Matiang’i, Boinnet na Kihalangwa kwa vile wote wamekaidi agizo la hii mahakama.

“Je, Matiang’i na wenzake wako wapi. Uliwaambia wanatakiwa kufika hapa kortini?” Jaji Odunga alimwuliza.

“Sikuwafikia kwa simu. Nilipiga simu mara 16 na sikujibiwa,” alisema Mutinda.

Bw Mutinda alijililia na kuomba korti isiamuru akome kutoa huduma za uwakili katika afisi ya mwanasheria mkuu ama kama wakili wa kibinafsi.

“Naomba hii mahakama iwachukulie hatua Matang’i, Kihalangwa na Boinnet. Nihurumie. Mimi ni wakili tu na kamwe sijakaidi agizo ka mahakama,” alijitetea Murinda.

You can share this post!

Kiburi cha Matiang’i, Boinnet na Kihalangwa...

Orengo ataka Miguna aundiwe pasi maalum ya usafiri...

adminleo