• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
Korti yamzuia DCI kufunga akaunti za kampuni ya pombe na mvinyo

Korti yamzuia DCI kufunga akaunti za kampuni ya pombe na mvinyo

Na RICHARD MUNGUTI

BIASHARA katika kiwanda cha kutengeneza pombe na mvinyo cha Africa Spirits na kampuni zingine nane zitaanza kutengeneza bidhaa baada ya Mahakama Kuu kuamuru akaunti zao zifunguliwe.

Na wakati huo huo, Jaji Luka Kimaru alimkosoea mkurugenzi wa uchunguzi wa jinai (DCI) kwa kujiingiza katika uchunguzi wa masuala ya ukwepaji ushuru.

Jaji Luka Kimaru aliyefutilia mbali agizo alilokuwa amepata la DCI kuchukunguza akaunti za kampuni tisa za bwanyenye Humphrey Kariuki, Jaji alisema mamlaka ya ushuru nchini (KRA) ina mamlaka na nguvu tosha za kuchunguza maswala ya ushuru bila kushirikisha polisi.

Jaji Kimaru aliiamuru KRA ichunguze masuala ya ushuru bila kumtegemea DCI jinsi sheria inavyoitaka.

Na wakati huo huo, Jaji Kimaru alifutilia mbali agizo la kufungwa kwa akaunti za kampuni tisa zikiwamo Africa Spirits Limited (ASL) na Wow Beverages Limited (WBL) zinazomilikiwa na Bw Kariuki.

Bw Kariuki na washukiwa wengine tisa wamekanusha mashtaka ya kukwepa kulipa ushuru wa Sh41 bilioni, kumiliki ethanol yenye thamani ya Sh7.9 milioni na kupatikana na risiti feki za ushuru.

Jaji Kimaru alikuwa ameombwa na mawakili Cecil Miller na Macmillan Ouma afutilie mbali agizo la mahakama ya Kiambu ya kufungwa kwa akaunti za makampuni tisa ya Bw Kariuki.

Akitoa uamuzi Jaji Kimaru alifutilia agizo la kufungwa kwa akaunti hizo akisema, “ Amri iliyotolewa na mahakama ya Kiambu ni kuchunguzwa kwa akaunti za kampuni tisa katika benki za Kenya Commercial (KCB) na National (NBK).”

Jaji huyo alisema kile polisi wameruhusiwa kufanya ni kuchunguza akaunti za mshukiwa na wala sio kuzifunga.

“Kwa mujibu wa sheria za KRA, maafisa wake wana uwezo na mamlaka ya kuchunguza akaunti na wala sio kuwaalika polisi kutenda yasiyowapasa,” alisema Jaji Kimaru.

Jaji aliamuru kesi iliyowasilishwa na DCI katika mahakama ya Kiambu iwasilishwe mbele yake kuisoma na kisha kutoa maagizo yanayofaa.

Kuhusu kusitisha kusikizwa kwa kesi alizoshtakiwa Bw Kariuki na wenzake, Jaji Kimaru alisema Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP) na KRA wanaweza endelea nazo.

You can share this post!

Mary Wambui ateuliwa serikalini

TAHARIRI: Kaunti zishughulike kuyakabili mafuriko

adminleo