• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 12:15 PM
Wazee wa Kaya wamuombea Sonko, waunga mkono BBI

Wazee wa Kaya wamuombea Sonko, waunga mkono BBI

Na FADHILI FREDRICK

WAZEE wa Kaya eneo la Pwani walimfanyia Gavana wa Nairobi Mike Sonko maombi maalumu katika eneo takatifu la Kaya Kinondo mnamo Jumamosi.

Wakiongozwa na Mwenyekiti wa Chama cha Wazee wa Kaya za Mijikenda, Bw Abdallah Ali Mnyenze, walimtetea Bw Sonko kwa masaibu yanayomkumba katika Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC).

Walidai gavana huyo anaandamwa na wafanyabiashara tapeli ambao wanataka kumharibia sifa zake za kuwa katika mstari wa mbele kupambana na ufisadi kaunti hiyo.

“Amekuwa akifichua sakata za ufisadi na tunashangaa kwa nini amegeuzwa kuwa mshukiwa,’ akasema.

Katibu wa chama hicho, Bw Juma Hamisi Mwakavi alisema wameamua kumtetea kwa sababu yeye ni mkazi wa Pwani anayeheshimu sana tamaduni za Wapwani.

Wakati huo huo, wazee hao wameapa kuunga mkono na kupigia debe ripoti ya jopo la maridhiano (BBI) itakapowasilishwa rasmi kwa umma.

Ripoti hiyo iliyoandaliwa na jopo la maridhiano ingali inasubiriwa kuwasilishwa kwa Rais Uhuru Kenyatta.

Wakiongozwa na mwenyekiti wao wa baraza la wazee wa kaya Bw Abdallah Ali Mnyenze walisema ripoti hiyo ambayo ilitokana na kukusanywa kwa maoni kwa wananchi itaisaidia Kenya kuwa nchi yenye utulivu na amani.

Wakihutubia wanahabari katika kaya ya Kinondo huko Diani, Kaunti ya Kwale, Bw Mnyenze alisitiza umuhimu wa mageuzi ya kikatiba nchini ili kuleta usawa kwa kila jamii nchini.

Alisema anamatumaini jopo hilo likusanya maoni ya wakenya na litazingatia maoni hayo kuleta mabadiliko nchini bila ubaguzi wowote.

‘Tuko tayari kuunga mkono ripoti hiyo ambayo tuna uhakika imezingatia maoni ya wakenya,’ akasema.

Katibu wa wazee hao wa kaya Bw Hamisi Juma Mwaviko alitoa wito kwa Wakenya kuiunga mkono ripoti ya BBI akisema italeta manufaa kwa wananchi kwani ripoti hiyo natokana na mkusanyiko wa maoni ya wakenya wa kila tabaka.

Bw Mwaviko alisema ripoti hiyo itakapotolewa rasmi lazima kuwe na uhamasisho zaidi kwa wananchi kujua kweli mapendekezo hayo yalizingatia maoni ya wakenya.

‘Kuna uwezekano katiba huenda ikarekebishwa lakini tunaomba hamasisho mashinani ili kueleza ripoti hiyo imependekeza nini,’ akasema.

Bw Mwaviko alisema kumekuwa na tetesi katika ripoti hiyo ambayo haijayolewa rasmi na hivyo kuomba baadhi ya viongozi kutowapotosha wakenya.

Na naibu mwenyekiti la baraza hilo Bw Stanley Kenga alisema kama wazee wa kaya wanaunga juhudi za kuwapatanisha wakenya kupitia jopo la maridhiano na kuwasihi wananchi kusubiri mapendekezo la jopo hilo.

‘Tutapigia debe ungwaji mkono kwa mapendekezo hayo katika ripoti hiyo ya BBI endapo kutakuwa na mapendekezo ya kurekebisha baadhi ya vipengele katika katiba,’ akasema.

Hatua hiyo ya wazee hao wa kaya kuunga mkono ripoti hiyo yanajiri huku joto likizidi kupanda kuhusu ripoti hiyo ambayo haijatolewa rasmi.

Magavana pia wana mchakato wao wa marekebisho ya katiba ambao ni Ugatuzi Initiative kwa lengo la kuimarisha serikali za kaunti.

You can share this post!

Wazee walia kunyimwa hela za uzeeni

Hasara unga wa Dola kupigwa marufuku

adminleo