• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 8:55 PM
Buffon: Michael Oliver ana jaa la taka rohoni, alifaa kula vibanzi na mashabiki

Buffon: Michael Oliver ana jaa la taka rohoni, alifaa kula vibanzi na mashabiki

Na CHRIS ADUNGO

KIPA wa Juventus Gianluigi Buffon alimkejeli kwa kila aina ya maneno mazito refarii Michael Oliver baada ya timu yake kuaga mashindano ya Klabu Bingwa Ulaya mikononi mwa Real Madrid.

Juventus ilijitahidi na kufunga mabao matatu, hali iliyosawazisha mabao ya jumla na kuwa 3-3 baada ya Mario Mandzukic kufunga mabao mawili na moja la Blaise Matuidi.

Lakini robo fainali hiyo iliamuliwa katika muda wa ziada baada ya dakika 90 kukamilika ambapo Cristiano Ronaldo alifunga penalti, baada ya kipa huyo mwenye miaka 40 akilishwa kadi nyekundu kwa kupinga vikali uamuzi wa kuipa Real Madrid penalti.

“Refarii anayejua kazi yake hawezi kuharibu ndoto ya timu ambayo imejitolea kwa jino na ukucha kwa dakika 90,” alichemka alipohojiwa na wanahabari.

“Binadamu hewazi kupiga filimbi katika tukio lenye shaka kama hilo, anaweza tu ikiwa ana jaa la taka ndani ya roho yake. Ikiwa hauna heshima yako mwenyewe, unafaa kuketi kule kwa mashabiki na kula vibanzi ukiwa na familia yako. Refa wa mechi hii hakuwa ametimu kuichezesha katika ngazi hii.

“Ningemwambia refa huyo kila aina ya neno baya wakati huo, lakini alifaa kuelewa kiwango cha hatari aliyokuwa akileta. Ikiwa hauwezi kufanya uamuzi wa ujasiri, basi unafaa kujumuika na mashabiki na ule vibanzi.

“Ikiwa hauna sifa zifaazo katik viwango vya juu, ni bora kwako utazame mechi ukiwa na mkeo na watoto mkila vibanzi kwa viti vya mashabiki. Ni swali la uzito wa hali ambao kila mja anafaa kuwa nao, kujua utachezesha mechi au la. Inamaanisha kukosa kujua msimamo wako na timu zinazocheza. Kwa ufupi, inamaanisha hujui lolote,” cheche za maneno zikamtoka Buffon.

 

You can share this post!

Juventus yakabiliana na Real Madrid baada ya penalti chungu

WATOTO: Bingwa wa uogeleaji

adminleo