• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:33 AM
DINI: Liwezalo kufanywa leo lichangamkie sasa hivi!

DINI: Liwezalo kufanywa leo lichangamkie sasa hivi!

Na FAUSTIN KAMUGISHA

KUNA methali ya Kiyahudi isemayo, kama sio sasa ni lini? Kama sio sisi ni nani?

Katika makala haya tutazungumzia sehemu ya kwanza ya methali hii: Kama sio sasa ni lini?

Liwezekanalo sasa lisingoje saa ijayo. Liwezekalo leo lisingoje kesho.

“Sasa ndio wakati wa neema.” (2 Wakorintho 6:2). Sasa ni baraka. Sasa ni neema. Sasa ni fanaka. Sasa ni bahati. Sasa ni majaliwa ya Mwenyezi Mungu.

Nafasi ya kujaribu tena inaitwa sasa. Sasa iwe ndefu au fupi, ni muda. Sasa ni fursa. Ni kama fimbo, iwe ndefu au fupi ni fimbo. Mtu awe mrefu au mfupi, ni mtu.

Sasa ni wakati uliopo, muda huu, kinyume cha baadaye. Sasa ni wakati wa kuanza uliloamua kulifanya. Sasa ni wakati wa kuwa na nidhamu ya kumalizia ulilolianza.

Unataka kuwa na elimu ya juu, kama sio sasa ni lini? Unataka kufungua biashara, kama sio sasa ni lini? Unataka kuvunja rekodi yako ya mwaka jana, kama sio sasa ni lini? Unataka kupima afya yako, kama sio sasa ni lini? Unataka kuwa na vyanzo vingi vya pesa, kama sio sasa ni lini? Unataka kuwa mcha Mungu, kama sio sasa ni lini? Unataka kuwa na pasipoti, kama sio sasa ni lini? Unataka kuweka akiba ya pesa kwa ajili ya kesho isiyojulikana, kama sio sasa ni lini?

Methali ya China inatuasa, “Usiogope kutembea polepole, ogopa kusimama tu.” Ni kama methali nyingine isemayo, maji yanayotiririka hayachafuki. Maji yakituama kwenye dimbwi baadaye yananuka.

Unapopiga hatua ni bora kuliko kuwa na kigugumizi cha maamuzi au maendeleo. Huwezi kununua inchi ya muda kwa inchi ya dhahabu. Muda ukipita, umepita. Kuwa na mti wa kijani moyoni na pengine ndege anayeimba atakuja. Kwa ufupi jiandae.

“Fursa inapokuja, unakuwa umechelewa sana kujiandaa” alisema John Wooden, mchezaji wa mpira wa kikapu. Jiandalie fursa kabla ya fursa kugonga hodi. Fursa ipo mikononi mwako ichangamkie sasa.

Sasa ni mwanzo. “Chochote unachokipenda kifanye sasa, muda hauko upande wako,” alisema Marty Rubin.

Wakati wa kuamka toka usingizi wa “nitafanya kesho” ni sasa. Muda wa kutumia teknolojia ni sasa.

Katika sasa kuna uwezekano usio na kikomo. Ukiishi katika sasa mambo mengine yatajipanga. Jana huwezi kuibadilisha, kesho bado ni ndoto.

Kuna hadithi juu ya mtu ambaye aliandika wosia kumrithisha shetani nyumba, shamba na kibanda chake. Hakimu alitoa hukumu hii: “Liache shamba liote magugu. Udongo umomonyoke. Acha nyumba iharibike na miti ya kibanda ioze. Kutofanya lolote hiyo tayari ni kumrithisha shetani. Fanya kitu sasa. Panga na tekeleza mpango.”

Kupanga ni kuleta wakati ujao katika wakati uliopo ili kufanya kitu juu yake,” alisema Alan Lakein.

Kusitasita ni adui wa kufanya mambo. Kuna methali ya Wahaya isemayo, “Wamekupa habari za msiba wakati wa kiangazi umeenda msibani wakati wa masika.”

Wenye kusitasita hupigiwa methali hii. Jambo linalostahili kutendwa papo hapo lisipotendwa kwa wakati ufaao, hutia hasara.

“Adui wetu wa kweli maishani ni ‘ingekuwa’ na ‘kama’. Wanatuvuta nyuma ili tuingie wakati uliopita usioweza kubadilishwa, na mbele wakati ujao usiotabirika. Lakini maisha halisi yanachukua nafasi papa hapa na kwa sasa,” alisema Padre Henri Nouwen. Majuto ni mjukuu, mwishowe huja kinyume.

Kujipanga ni sasa. Ukarimu ni sasa. Kuwekeza ni sasa. Kujitathmini ni sasa. Kujiendeleza ni sasa. Kuwa mtu wa watu ni sasa. Kuwa na vipaumbele ni sasa. Kuacha jina zuri ni sasa. Ukianza jambo zuri usiliache bila kulikamilisha.

You can share this post!

Kabras Sugar yatumia uwanja wa nyumbani vyema kwa kuipiga...

KINAYA: Hapa kwetu, BBI na kukabili upinzani ni muhimu...

adminleo