• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 3:34 PM
Munya asuta viongozi kwa kuzindua miradi hewa

Munya asuta viongozi kwa kuzindua miradi hewa

Na DAVID MUCHUI

WAZIRI wa Kilimo, Bw Peter Munya amelaumu viongozi wakuu serikalini ambao wamekuwa wakianzisha miradi mipya kila mara kwa kufanya miradi mingi ya kitaifa ionekane imekwama.

Huku akionekana kumlenga Naibu Rais William Ruto ambaye wakati mwingi huzindua miradi katika ziara zake pembe tofauti za nchi, Bw Munya alisema huwa ni makosa kwani pesa hazijatengwa kwa miradi mingine inayozinduliwa.

“Miradi kadhaa ilizinduliwa hata kabla pesa kutengwa. Umeona watu wakizungukazunguka na kutangaza kuwa ‘tunatenga hapa, tunatenga pale, kule’. Baadaye, mradi husimama hadi pesa zitengwe kwa njia sahihi. Hii ni shida kubwa na tunajua,” Bw Munya alisema.

Hii inakuja baada ya Rais Uhuru Kenyatta, wiki tatu zilizopita, kutangaza kwamba atakagua miradi ya serikali mwenyewe, akiwalaumu viongozi ambao hakuwataja, kwa kumsaliti.

Akizungumza eneo la Mikinduri, wakati wa mazishi ya mwakilishi wa wodi, Bi Petronilla Gainchi mnamo Jumamosi, Bw Munya alisema viongozi wengine wa serikali wamekuwa wakikosea kuzindua miradi kabla ya kupangwa, ili wasifike.

“Serikali inatafuta miradi iliyokusudiwa na tunatafuta pesa za kukamilisha barabara zilizosimama. Rais anashughulikia suala hilo. Tunajua miradi mingine ilipewa watu ambao hawawezi kazi,” alisema.

Waziri alisizisitiza kuunga mkono nafasi zaidi katika serikali kuu kupitia mpango wa BBI akisema itaimarisha nchi wakati wa uchaguzi.

Rais Uhuru Kenyatta aliwalaumu wawakilishi wake kwa kuishi kama mafisi.

Kuhusu Mpango wa Maridhiano (BBI), Bw Munya alisema wale wanaopinga wanapaswa kujifunza kuishi nayo.

Alisisitiza kuwa BBI ilikusudiwa kuleta amani na utulivu nchini na kuongeza kuwa simulizi zinazoshirikishwa na wapinzani wake zilikuwa zinasimulia hadithi.

“Rais na Bw Odinga walikutana pamoja kuiunganisha nchi kwa ustawi. BBI imekusudia kumaliza uhasama na kujenga mazingira mazuri ya biashara na mafanikio ya kiuchumi ya kijamii,” akasema.

Akaongeza: “Zingine ni hadithi. Wale wanaodai kuwa kuna watu wa kumzuia mtu kutoka kwa kuwania urais sio kweli. BBI inastahili kumaliza uhasama unaohusishwa na uchaguzi.”

Vilevile, aliongeza kuwa ugatuzi umeshindwa katika kuponya uhasama wa kikabila na umoja kwa hivyo kulikuwa na haja ya mbinu mpya katika uongozi wa kitaifa.

Bw Munya aliwataka viongozi wote kuhudhuria mkutano wa hadhara uliowekwa wa BBI wikendi ijayo huko Meru ili kuhakikisha maoni yote yamechukuliwa.

“Nina uhakika mara tu yote haya yakifanyika, tutakuwa na kura ya maoni ya kurekebisha Katiba ili kuhakikisha mabadiliko ya amani na uchumi,” akasema.

Kadhalika, aliingilia siasa za Meru akisema viongozi hawachukulihi malalamishi ya wapinzani wao kwa uzito.

You can share this post!

Sonko atimua kaimu katibu

TAHARIRI: Idadi ya watu isizidi maendeleo ya nchi

adminleo