• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
AKILIMALI: ‘Ninaunda maelfu kutokana na uchoraji’

AKILIMALI: ‘Ninaunda maelfu kutokana na uchoraji’

NA MARGARET MAINA

[email protected]

Bw Robert Chumbi, 28 huvutia wapita njia na picha alizochora.

“Kama msanii, moja ya njia bora za kuonyesha talanta zako ni kwenye turubai. Kutoka kwa uchoraji wa rangi za mafuta hadi picha za turubai, kuna kitu tu juu ya nyenzo hii ambayo inaipa hisia ya ufahari,” anasema Robert

Mzaliwa wa Nanyuki, Robert anasema kwamba baada ya shule ya upili alianza kuuza viatu jijini Nairobi kujipatia riziki lakini baadaye alihamia Mombasa kukarabati pikipiki na baadaye kuwa wakala wa nyumba.

Lakini shauku yake ya sanaa hayakumruhusu kuzingatia mambo mengine na mnamo 2012 alirudi Nairobi na kupitia rafiki yake, alijifunza kutengeneza sanamu za wanyama.

“Nilianza kuchora vitu tofauti kwa kutumia penseli kutoka umri mdogo. Na ingawa nilijifunza kuchonga sanamu za wanyama, mapato hayakuwa nzuri kwani haukua na soko nzuri na ulichukua muda kwa sanamu kukauka, “anasema.

Robert aliamua kuhamia kabisa kwenye turubai uamuzi ambao hajuti.

“Nilikuwa na pahali pa kuonyesha sanaa yangu Kinoo lakini nilikuwa nikisafiri kwenda Nakuru kuuza vipande vyangu na faida ilikuwa ya kuvutia .”

Bw Robert, pamoja na rafiki yake Samwel Kinuthia walihamia Nakuru Januari 2019.

Bw Robert ambaye sasa ana wafanyikazi watatu anasema kwamba huviuzi uchoraji wao kuanzia Sh 1,000 hadi Sh 15,000 na kupata faida wa angalau Sh 60,000 kwa mwezi mzuri. Lakini pia anakumbana na changamoto tofauti.

“Tunafanya kazi nje na wakati kunanyesha lazima tufunge kazi. Hii inasababisha uchoraji wetu kuchukua muda mrefu kukauka,’’anasema

Wateja wake ni kati ya wanasiasa na mwananchi wa kawaida na hii imemfanya Robert kuwa mbunifu zaidi .Huwa pia anawalenga watalii walio njiani kuelekea ziwa Bogoria.

Anatarajia kuwa na studio katika siku zijazo na kupanua soko lake kwa miji tofauti.

“Katika tasnia hii, ni muhimu sana kwa wasanii kupata msaada na ushauri kutoka kwa wasanii wakubwa kwani ni rahisi mtu kukata tamaa.”

You can share this post!

AKILIMALI: Usanii wa kurembesha mifuko unalipa

Afueni kwa wafanyabiashara baada ya soko kufunguliwa

adminleo