• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 7:50 AM
MJI WA KALE: Serikali yaruhusu shughuli za wafanyabiashara katika bandari ya zamani

MJI WA KALE: Serikali yaruhusu shughuli za wafanyabiashara katika bandari ya zamani

Na WINNIE ATIENO

AFUENI kwa wafanyabiashara wanaotegemea bandari ya zamani maarufu Old Port iliyoko Mji wa Kale – Old Town – baada ya serikali kuwaruhusu kuendeleza shughuli zao licha ya kufungwa kwa eneo hilo.

Serikali ilifunga eneo hilo hivi majuzi ili kupunguza maambukizi ya virusi vya corona katika Kaunti ya Mombasa.

Wakazi wa Mji wa Kale wanaongoza kwa maambukizi ya virusi vya corona na kifo kutokana na ugonjwa wa Covid-19 katika Kaunti ya Mombasa.

Mshirikishi wa eneo la Pwani John Elungata na Waziri msaidizi wa Maswala ya Ndani – CAS Interior – Bw Hussein Dado wamewapongeza wakazi kwa kujitolea kupimwa kubainisha hali yao ikiwa wana Covid-19 au la.

Kati ya watu 17 walioaga dunia kufuatia ugonjwa huo Kaunti ya Mombasa tisa wanatoka Mji wa Kale.

“Tumekuja kutathmini mabadiliko tangu serikali ifunge eneo hili; tunafurahi kuona kwamba watu wamekubali kupimwa na wanaendelea kutii utaratibu uliowekwa na hata kukaa nyumbani isipolazimu watoke. Tunaona mafanikio na tukiendelea hivi malengo yetu ya kupunguza maambukizi yaliyokuwa yamekita mizizi yatatimia,” alisema Bw Elungata.

Naye Dado aliwataka ‘wanaojificha’ wajitokeze ili wapimwe.

“Ni vizuri upimwe ujue hali yako. Tumekuja kuangalia changamoto wanazopitia wakazi hapa. Msisikize porojo za watu wa huko nje; tufuate taratibu za serikali,” alisema Bw Dado.

Alisema mzigo iliyokuwa imekwama katika bandari iliyoko Mji wa Kale kufuatia kufungwa kwa eneo hilo itaruhusiwa kupakuliwa.

“Tulipata habari kutoka kwa wafanyabiashara wakisema mizigo yao iko tayari kuondoka katika bandari hii lakini mahamali wamekatazwa. Lakini sasa kupitia kwa Bw Elungata, mahamali watapewa nafasi ya kuingia na kupitisha mizigo ili biashara iendelee,” alisema Bw Dado.

Njia za kukwepa vizuizi

Wakati huo huo, Bw Elungata alisema maafisa wa usalama wamefunga njia zote za mikato ambazo wakazi walikuwa wanatumia kutoka au kuingia kaunti za Mombasa, Kilifi na Kwale.

Hata hivyo, aliwataka wakazi kuwasema wanaoingia na kutoka kaunti hizo.

You can share this post!

Visa vya maambukizi ya Covid-19 vyagonga 700

‘Huenda ukalazimika kupimwa Covid-19 kabla ulazwe...

adminleo