• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 3:25 PM
Wanafunzi wa vyuo vya ufundi Garissa waanzisha mradi wa utengenezaji barakoa

Wanafunzi wa vyuo vya ufundi Garissa waanzisha mradi wa utengenezaji barakoa

Na FARHIYA HUSSEIN

WANAFUNZI katika vyuo vya ufundi Kaunti ya Garissa wameanzisha mpango wa utengenezaji barakoa kusaidia katika mapambano dhidi ya janga la Covid 19.

Wanafunzi hao kufikia sasa wametengeneza barakoa zaidi ya 50,000 katika kipindi cha wiki mbili.

Afisa Mkuu wa elimu katika kaunti hiyo, Bw Mohammed Gure amethibitisha.

“Utenegenezaji wa barakoa hizi unafanyika katika chuo cha ufundi cha Garissa. Lengo kuu ni kusambaza barakoa katika maeneo yanayokubwa na uhaba kwenye kaunti hii,” Bw Gure akasema.

Amesisitiza kwamba wakipata mashine za kutengezea vifaa hivyo na msaada unaofaa wanaweza kutengeneza barakoa zaidi ya 100,000 kwa mwezi mmoja.

“Shughuli hiyo inaendelezwa na kikosi kutoka vyuo vya mafunzo ya kiufundi vya Bura, Mkono na Garissa. Tayari tumefanikiwa kutengeneza na kusambaza barakoa 50,000. Hii itasaidia sana katika kupambana na ugonjwa wa Covid-19,” afisa mkuu huyo alisema.

Watakaofaidi zaidi ni waathiriwa wa mafuriko katika kambi za IDP, hospitali, magereza na sehemu nyinginezo za kijamii ambazo zinakisiwa kuwa dhaifu.

“Tumekuwa katika kituo hicho na tumevutiwa sana. Tunashukuru juhudi kutoka kwa timu hiyo. Tunawaunga mkono na tutawapa msaada kutoka upande wetu,” Bw Gure akaahidi.

Timu hiyo iliongozwa na wakuu wa vyuo hivyo vya elimu ya kiufundi akiwemo Bw Ahmed Hassan wa chuo cha mafunzo ya kiufundi, Bi Amina Hassan kutoka Chuo cha Biashara, Ufundi na Kazi za Mikono na Bw Osman Abdi Ali wa Chuo cha Ufundi cha Bura.

Bw Gure pamoja na Mkurugenzi wa mafunzo ya ufundi Bw Hassan Yarrow na Mkurugenzi Msaidizi Mohamed Noor wamehakikishiwa kuwa vifaa vilivyotumika vilikuwa vya ufanisi na vya kisasa kulingana na mahitaji ya Shirika la Kukadiria Ubora wa Bidhaa (Kebs).

“Waathiriwa wa mafuriko ambao wanaishi katika kituo cha mafunzo ya ufundi tayari wamepokea barakoa hizo za bure zanazotengenzwa katika kituo hicho,” alisema Gure.

Wakati huo huo, timu ya wataalamu wa mabomba na ile ya ujenzi kutoka kwa vyuo hivyo vya ufundi wamevumbua kifaa cha kunawa mikono (hand sanitizer dispenser).

You can share this post!

Nimefanyia wanasoka wa Harambee Stars mambo mengi makubwa...

TAHARIRI: Serikali iunge juhudi za kuwalinda watoto

adminleo