• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 3:04 PM
Weta kuadhibu waliobadilisha uongozi chamani

Weta kuadhibu waliobadilisha uongozi chamani

BENSON MATHEKA na RICHARD MUNGUTI

CHAMA cha Ford Kenya kimebuni kamati itakayoamua hatua kitakachochukulia maafisa waliojaribu kufanya mapinduzi ya uongozi.

Kamati ya usimamizi wa chama hicho inayosimamiwa na Kiongozi wa Chama Moses Wetang’ula iliyokutana jana katika makao makuu jijini Nairobi iliamua kutumia mbinu za ndani kutatua mzozo wa uongozi chamani.

Mahakama kuu Jumatatu alasiri ilimzuia Msajili wa vyama vya kisiasa Anne Nderitu kumsajiili Wafula Wamunyinyi kuwa kinara wa Chama cha Ford-Kenya.

Jaji James Makau alipiga breki hatua ya Bw Wamunyinyi kunyakua uongozi wa Ford-Kenya akaamuru kesi kuhusu mzozo huo wa Ford-Kenya isikizwe Juni 29.

Alisitisha utekelezwaji wa Arifa ya Gazeti rasmi la Serikali ya Juni 8, 2020 iliyomtangaza Wamunyinyi kuwa kinara wa chama cha Ford-Kenya.

Ombi la kutotambuliwa kwa kundi la Wamunyinyi na Bi Nderitu liliwasilishwa na wakili Ben Millimo.

Ford Kenya sasa imeunda kamati ya kutatua mizozo inayosimamiwa na Naibu Kiongozi wa chama, Bw Richard Onyonka.

Katibu Mkuu Eseli Simiyu na Mbunge wa Kanduyi Wafula Wamunyinyi wanatarajiwa kuhojiwa na kamati nyingine ya nidhamu inayosimamiwa na Mbunge wa Mugirango Magharibi Vincent Kemosi.

Bw Simiyu analaumiwa kwa kumuondoa Bw Wetang’ula kama kiongozi wa chama. Kulingana na Seneta huyo wa Bungoma, Simiyu aliita mkutano haramu wa baraza kuu la kitaifa la chama kutekeleza mapinduzi.

Kamati simamizi ya chama ilipitisha kwamba Bazara Kuu la Kitaifa ya chama hicho itakutana hivi karibuni kuandaa mkutano wa wajumbe watakaochagua viongozi wapya.

Bw Onyonka aliyehudhuria mkutano wa jana alikariri uaminifu wake kwa chama na Bw Wetangula. Mbunge huyo aliahidi kutatua mzozo huo kwa kuzingatia katiba ya chama.

Chama hicho kilitangaza kitaandaa mkutano wa Kamati Kuu ya chama (NEC) hivi karibuni ili kuanzisha mipango ya kupanga uchaguzi wa viongozi wapya chamani.

You can share this post!

Yafichuka ODM ilipanga kuiba kura 2007

Wasichana 28 hupachikwa mimba kila siku Machakos –...

adminleo