• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 3:03 PM
Sukari ya Sh5 bilioni kusalia bandarini

Sukari ya Sh5 bilioni kusalia bandarini

Jaji Mkuu David Maraga, naibu wake Philomena Mwilu, Majaji Mohammed Ibrahim, Smokin Wanjala na Isaac Lenaola wakati wa kesi. Picha/ Richard Munguti

Na RICHARD MUNGUTI

MAMLAKA ya ushuru nchini KRA Jumanne iliamriwa isiondoe sukari ya Sh5 bilioni katika bandari ya Mombasa.

Mahakama ya Juu iliagiza sukari hiyo iliyoingingizwa nchini Novemba 2017 isalie bandarini Mombasa hadi rufaa iliyowasilishwa na kampuni iliyoingiza sukari hiyo kutoka Brazil isikizwe na kuamuliwa.

Jaji Mkuu David Maraga, naibu wake Philomena Mwilu, Majaji Mohammed Ibrahim, Smokin Wanjala na Isaac Lenaola walisema ni muhimu kuzuia KRA kutwaa sukari hiyo kabla ya ukweli  kubainika.

Lakini kampuni ya Darasa Investments Limited ilisema ilikuwa imelipa ushuru wa zaidi ya Sh422 milioni na kwamba, KRA ilipasa kuiruhusu iuze sukari hiyo.

Darasa iliingiza Sukari hiyo humu  nchini mnamo Novemba 2017.

Kampuni hiyo inaomba mahakama iamuru Serikali iilipe Sh5bilioni ikiwa ni hasara ambayo imepata kwa kuendelea kuzuilia sukari hiyo.

Isitoshe, Darasa inaomba uamuzi wa Majaji Alnashir Visram, Wanjiru Karanja na Martha Koome ufutiliwe mbali na iruhusiwe kuondoa sukari yake kutoka bandari ya Mombasa iuze.

“Baada ya kusikiliza ushahidi wa Darasa kupitia kwa wakili Mansur Issa, hii mahakama inakubali kuwa kuna masuala mazito ya kisheria yanayopasa kuamuliwa kabla ya sukari hiyo kuachiliwa kutoka bandarini,” walisema majaji hao wa Mahakama ya Juu.

Majaji Visram, Karanja na Koome wa Mahakama ya Rufaa waliamuru KRA ifanye hesabu ijue kiwango cha kodi ambacho Darasa ilitakiwa ilipe.

KRA ilitakiwa ifuate sheria iliyochapishwa katika Gazeti rasmi la Serikali ya Mei 12, 2017 na kufanyiwa marekebisho mnamo Oktoba 4, 2017.

Kampuni hiyo ilikuwa inaomba KRA ishurutishwe kuilipa fidia ya $8milioni (832,000,000) kwa sababu ya kukataa kuiruhusu iondoe sukari hiyo kutoka bandarini.

Pia, Darasa ilikuwa imeomba korti iamuru KRA ilipe ada zote za kuhifadhiwa kwa sukari hiyo tangu iingizwe humu nchini na meli ijulikanayo  kama NV Iron Lady,

Pia, iliomba korti iamuru ikubaliwe kuondoa  sukari hiyo bandarini pasi na kulipia ushuru wa forodha.

Majaji Visram, Karanja na Koome walisema kulikuwa na stakabadhi mara mbili kuhusu kuingizwa kwa sukari hiyo ya tani 40,000 kutoka nchini Brazil zilizokuwa zinakanganya.

You can share this post!

Kalameni amtoroka slay queen akihofia hasara zaidi

Sura mpya ya ‘Baba’ baada ya salamu

adminleo