• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 1:15 PM
Serikali kukata rufaa ya uamuzi kuhusu Pasta Ng’ang’a

Serikali kukata rufaa ya uamuzi kuhusu Pasta Ng’ang’a

Na AGEWA MAGUT

KUTOKANA na kuachiliwa huru kwa Mchungaji James Maina Ng’ang’a aliyeshtakiwa kwa ya mauaji barabarani, Waziri wa Usalama wa Ndani Fred Matiang’i Jumanne alisema atakata rufaa huku Wakenya wakizidi kulalamika.

Katika barua, Dkt Matiang’i aliagiza Mwendeshaji wa Mashtaka ya Umma, Noordin Haji kukata rufaa ya kesi hiyo ambapo Bw Ng’ang’a alishutumiwa kwa kuendesha gari vibaya na kusababisha kifo.

Kulingana naye, kuna ushahidi wa kutosha wa kuendesha kesi hiyo.

“Niwaomba kukata rufaa na kuwatafutia haki waathiriwa na wananchi wa Kenya,” alisema Dkt Matiang’i kwenye barua.

Wakenya walikasirishwa na hatua ya mahakama kumwachilia huru Mhubiri Ng’ang’a baada ya kushtakiwa kwa kuua mwanamke kwa kuendesha gari vibaya miaka mitatu iliyopita.

Watumiaji wa mtandao wa Twitter walielezea kutoridhishwa na mahakama na kuonekana kukata tamaa baada ya mchungaji huyo kuwekwa huru na mahakama moja ya Limuru mnamo Jumatatu.

Wakenya wengi walioneka kumkashifu Jaji Mkuu David Maraga, ambao wanaamini kuwa amepuuza kinachoendelea katika Idara ya Mahakama.

“Ni kumaanisha kuwa haki katika mahakama zetu ni kwa matajiri pekee? Watu maskini wanaweza kupata haki kweli katika mahakama zetu zilizooza,” aliuliza Victor Achochi.

“Baba mkwe wa mwendazake aliuliza: “Kuachiliwa huru kwa washtakiwa ni kumaanisha watoto wangu walitayarisha ajali iliyosababisha mauti ya mkwe wangu?” Hilo ni swali la haki, familia lazima itakata rufaa uamuzi huo wa mahakama,” alisema Joe Muhahami.

Wengine walisema kuwa uendeshaji wa mashtaka ndio ulikuwa na shida lakini haikuwa hakimu aliyetoa hukumu hiyo.

Wengine waliwashutumu maafisa wa polisi, ambao baadhi yao hushirikiana na washtakiwa na kuchukua hongo kwa lengo la “kupoteza” ushahidi.

Katika kisa hiki, baadhi ya watu walioshuhudia ajali hiyo iliyotokea Julai 2015, walisema walimuona mhubiri huyo akiendesha gari hilo.

Hata hivyo, katika taarifa ya polisi, sehemu hiyo ya ushahidi haikurekodiwa. Hivyo, Hakimu Godfrey Oduor alitoa hukumu iliyompendelea mchungaji huyo kwa kukosa ushahidi wa kutosha.

Mwangi Francis aliandika, “Soma stakabadhi ya mashtaka, ni rahisi kusema kwamba imegeuzwa. NTV ilionyesha picha za leseni iliyokamilika muda wake ya Mchungaji Ng’ang’a. Mamlaka ya Uchukuzi na Usalama ilithibitisha kuwa alikuwa amelewa. Hadithi sasa imekuwa tofauti…”

Maskwel@Omogirango aliandika, “Majaji huwa hawafanyi uchunguzi, kabla ya kupiga kelele #JusticeForMercyNjeri, ninawaalika kukabiliana na waendeshaji mashtaka kwanza, ndio mtajua mahali na wakati kesi hiyo iliisha.”

Wengine walieleza aina ya maisha wanayoishi baadhi ya wachungaji kutokana na zaka na sadaka kutoka kwa wafuasi wao.

Paul Njogu alisema: “Utamaduni wa Kiafrika uliheshimu maisha ya binadamu, hakuna aliyeepuka haki.”

You can share this post!

Polisi wanatumiwa kututishia – Wahadhiri

Wabunge walia kuhangaishwa mitandaoni

adminleo