• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 12:32 PM
WALLAH BIN WALLAH: Jichunge, asilani usijigeuze ng’ombe wa kuchungwa

WALLAH BIN WALLAH: Jichunge, asilani usijigeuze ng’ombe wa kuchungwa

NA WALLAH BIN WALLAH

UNAPOAMBIWA chunga usifikirie tu kitendo cha kuwapeleka wanyama malishoni! Ama usidhanie ni kuchukua chungio au chekeche ili kuchunga unga au nafaka kuondoa chenga na takataka nyingine.

Chunga ujichunge, ujitunze, ujilinde na uyatazame mambo kwa macho ya tahadhari.  Chunga ujichunge usiwe kama ng’ombe mnyama ambaye lazima aelekezwe ndipo ajue pa kuenda kujilisha! Ujichunge sana kwa akili na maarifa!

Kaokote alikuwa na tabia aliyoijua yeye mwenyewe. Ilikuwa siri yake ambayo hakuna aliyeijua kuanzia wazazi wake, walimu wake hata mimi rafiki yake wa dhati!

Kaokote alikuwa na tabia ya kuokotaokota kila kitu alichokipata njiani au mahali popote pale! Alizoea kuokotaokota mpaka akawa na mazoea ya kuchukua vitu vya watu bila idhini!

Mtu akisahau au akiacha kitu chochote mahali, Kaokote hukiokota akaenda nacho! Kwa mujibu wa heshima zetu tu, hatupendi kumwita MWIZI!

Lakini kusema ukweli, Kaokote alikuwa MWIZI!Wazazi wa Kaokote walimshauri na kumkumbusha kila mara, ‘Mwanetu, tabia njema ndio usalama wa mtu duniani! Ujichunge! Usiwe na tamaa wala usivipende vitu vya bure, vya kupewa au vya kuchukuachukua kutoka kwa watu! Utakula sumu siku moja!

Vitu vingine vitakukwamia tumboni! Tumia akili! Fikiria sana kabla ya kuyatenda mambo! Majuto ni mjukuu! Tafadhali ujichunge!’Walimu nao huko shuleni waliwashauri wanafunzi kila mara wakisema, ‘Tabia njema ndiyo mafanikio na maendeleo ya kila mtu maishani!

Hata ukijaliwa kuwa na kila kitu maishani, lakini tabia zikiwa mbaya, ujue kila kitu ulicho nacho ni kibaya!’ Kaokote na wenzake waliyasikia hayo lakini hawakuyazingatia.Siku moja wazazi wa Kaokote waliondoka nyumbani kuenda kwenye matanga katika kijiji jirani!

Kaokote aliona amepata mwanya wa kuenda kuzurura! Alipokuwa njiani akienda alikoamua kuenda, karibu na msitu, aliona kikapu kikubwa kichafu kilichokuwa kando ya njia. Alisimama akatazama kila upande na hakumwona mtu yeyote karibu!

Kaokote akakiokota kikapu na kukibeba kichwani akapiga mbio kurudi nacho nyumbani! Alipofika nyumbani, alijifungia ndani ya chumba. A

kaanza kuyaondoa majani yaliyofunikiwa mdomo wa kikapu! Ghafla, chatu mkubwa alikiinua kichwa chake akamtemea Kaokote mate ya sumu machoni!

Kaokote akawa kipofu pale pale mpaka leo!Naam, hivyo ndivyo matendo yetu mabovu na tabia zetu mbaya za ujeuri zinavyotuletea maafa makubwa maishani!

Tujichunge na tuyachunge macho yetu ili tuyaone matendo yaletayo maafa na majuto kila uchao katika jamii na mazingira yetu ili tuyaepuke! Chunga! Ujichunge mwenyewe! Usingojee kuchungwa! Chunga uone usalama wako uko wapi?

You can share this post!

ODM yajiandaa kupinga refarenda kufanywa 2022

OLIMPIKI: Afisa ajitetea kashfa ya mamilioni

adminleo