• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 5:29 PM
CHOCHEO: Tendo la ndoa ni raha, si karaha

CHOCHEO: Tendo la ndoa ni raha, si karaha

Na BENSON MATHEKA

“MTU wangu amezidi siku hizi. Silali. Sijui hanjamu zake zimetoka wapi na akiendelea hivi sitaweza kuvumilia,” Ciku* alimweleza rafiki yake wa karibu.

Alisema mumewe huwa anamhangaisha kila usiku akitaka haki ya ndoa.

“Hata mchana akiwa nyumbani, huwa anataka uroda. Kusema kweli he is just too much. I cannot cope,” akasema.

Lakini kwa rafiki yake Sue* mambo ni tofauti. Mumewe hashughuliki naye na amekuwa pia akifikiria kumuacha.

“Unalalamika wengine tukilia. Heri wako anakupepeta hadi unaogopa kupepetwa. Wangu ni baridi. Huchangamkia shughuli mara moja kwa wiki na kuniachia kiu. Nafikiria kuchepuka lakini naogopa hatari huko nje na naona heri nimuache rasmi nikatafute sogora wa ngoma kama huyo wako,” Sue alimwambia Ciku.

Ingawa marafiki hawa walikuwa na ujasiri wa kufunguliana roho zao, wataalamu wa masuala ya mapenzi wanasema ni miongoni mwa wengi wanaoteseka baada ya viwango vyao vya utekelezaji wa tendo la ndoa kutofautiana na vya wachumba wao. Wanasema kuwa baadhi ya wanawake hujipata hawamudu makombora ya wachumba wao nao wanaume wanapata hawawezi kutoshana na hanjamu za viosha roho wao.

“Hii huwa inatokea mara nyingi ambapo watu hupata hawakimu mahitaji ya tendo la ndoa la wachumba wao. Ni jambo la kawaida lakini linaloweza kuvunja uhusiano wa kimapenzi,” asema mwanasaikolojia Jimmy Gitau wa Shirika la Abundant Love, jijini Nairobi.

Anasema kuna wanawake walio na damu moto kuliko wachumba wao na wanataka ngoma kila siku iwe mchana au usiku na pia kuna wanaume ambao kwao burudani chumbani ni kama mlo.

“Tatizo kubwa ni kwamba hii inasababisha mateso ya kisaikolojia kwa aliye ni kiwango cha chini cha cha uroda na inaweza kumkosesha furaha. Hivyo basi, wachumba wakigundua uwezo wao wa kula uroda unatofautiana, wanafaa kutafuta mbinu za kusawazisha bila kuchepuka au kuachana,” asema Gitau.

Watalaamu wanapendekeza wachumba kujadili suala hili kwa uwazi bila hasira.

“Kuketi chini na kuzungumza kunaweza kusuluhisha tatizo hili kwa sababu linaweza kumpata kila mtu,” asema Gitau.

Kulingana na Mwanasaikolojia David Ouko wa shirika la Liberty Center, mtaani Athi River, kuna watu wanaoamini kuwa ujasiri wa kutekeleza tendo la ndoa ni kulishiriki kila siku.

“Kwao huwa wanataka kudhihirishia wachumba wao kwamba wanawapenda bila kubaini kwamba wanawatesa. Mazungumzo yanaweza kuwafanya waelewe kuwa wanaweza kudhihirisha mapenzi kwa njia mbadala,” asema.

Anasema kwamba watu wanaweza kuonyeshana upendo kwa kutendeana mema, kuandamana katika hafla za kijamii na kupakatana bila kushiriki tendo la ndoa.

“Kwa kufanya hivi, wachumba wanaweza kusawazisha viwango vyao vya ulaji uroda kwa sababu wanaelewana zaidi na kuaminiana. Ajabu ni kuwa wasiofanya hivi huwa wanashuku wenzao wana mipango ya kando wakisita kuwalisha uroda,” asema.

Wataalamu wanasema watu wanapojadili suala hili huwa wanakubaliana jinsi ya kukidhi hanjamu zao bila kutesana.

“Iwapo mmoja anataka kuchovya asali kila siku na mwingine mara tatu kwa mwezi, wakijadiliana wanaweza kukubaliana iwe mara mbili kwa wiki,” asema Ouko.

Mtaalamu huyu anasema uwezo wa kucheza ngoma chumbani hutegemea umri, afya na dhana ya mtu.

Nita Karimi, mtaalamu katika shirika la Sure and Refined Counseling Services, jijini Nairobi anasema njia bora ya kuweka viwango vyao utekelezaji wa tendo la ndoa katika kiwango sawa kwa wachumba ni kuwa na ratiba ya kulishana uroda.

“Wakati wachumba wanapoweka ratiba ya kulishana asali, taharuki huondoka katika akili zao wakijiandaa kwa siku ya ngoma,” asema.

Hata hivyo anasema watu hawafai kutumia ratiba ya kufanya mapenzi kuwaadhibu wachumba.

“Kila kitu kinafaa kuwa kwa kiasi na ustadi. Lisha mwenzako uroda kwa kumjali sio kumwadhibu ukijua kuna siku nyingine mliyopanga kupandishana mizuka,” asema.

Kulingana na Karimi watu wakiweka ratiba ya kulishana asali na kuidumisha, hawawezi kuchokana. Anasema hii huwa inasawazisha hanjamu zao na kuwaweka katika kiwango kimoja wanapomenyana chumbani.

You can share this post!

MUTUA: Wafisadi hawana aibu tena, watafuna bila kupepesa...

Dkt Ruto na Murathe waendelea kupapurana hadharani