• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
Aibu kwa madiwani wa Nakuru kumeza mishahara ya bwerere kwa miezi sita

Aibu kwa madiwani wa Nakuru kumeza mishahara ya bwerere kwa miezi sita

Na FRANCIS MUREITHI

MISWADA minne muhimu kutoka kwa madiwani wa wadi mbalimbali katika Kaunti ya Nakuru haijawahi kushughulikiwa na kamati mbalimbali za bunge la kaunti hiyo kwa zaidi ya miezi sita sasa.

Madiwani wa Bunge la Kaunti ya Nakuru wamelaumu uongozi mbaya katika bunge hilo kuwa kiini cha kutojadiliwa kwa baadhi ya miswada hiyo iliyowasilishwa kwa kamati husika kuanzia Machi 2020.

Mnamo Julai 16, Spika wa Bunge la Nakuru, Joel Maina Kairu alihimiza madiwani kujadili miswada yote iliyowasilishwa na kupisha upesi mchakato wa kuundwa kwa sheria mbalimbali.

Kwa mujibu wa kanuni 123 na 125 za Bunge la Kaunti, miswada yote inayowasilishwa kwa kamati husika bungeni inastahili kujadiliwa na madiwani chini ya kipindi cha siku 20.

Haya yanafanyika wakati ambapo baadhi ya wakazi wa kaunti wameanza kupoteza imani na Bunge la Kaunti ya Nakuru ambalo kwa mujibu wao, limeshindwa kabisa kushughulikia majukumu muhimu ya uundaji wa sheria.

Mswada kutoka kwa Diwani wa Gilgil, Jane Ngugi kuhusu jinsi shamba la eneo la Kembi Somali litakavyotumika haujajadiliwa kwa muda mrefu kwa sababu mwenyekiti wa kamati ya Ardhi, Ujenzi na Mipango ya Miji, Stephen Ngethe Chege wa Maai Mahiu, hajawahi kufika bungeni kwa muda ikiwemo Oktoba 30 iliyokuwa siku ya kujadiliwa kwa mswada wake.

Naibu mwenyekiti wa kamati hiyo, Gladys Nyambura Kairu, ambaye ni diwani mteule, alisema mustakabali wa mswada huo utajulikana baada ya wiki mbili zijazo.

Kwa upande wake, diwani wa Naivasha Mashariki, Stanley Karanja alisema sheria nyingi kuhusu jinsi masuala ya Kaunti ya Bunge la Nakuru yanavyoendeshwa zimekiukwa.

“Kukosekana kwa miswada ya kujadiliwa bungeni na ile iliyowasilishwa kutojadaliwa sasa ni jambo la kawaida katika Bunge la Kaunti ya Nakuru. Huu ni mtindo wa kutisha na ni ishara kwamba Kamati ya Masuala ya Bunge imetepetea,” akasema Karanja katika kauli iliyoungwa mkono na Kaimu Spika wa Bunge, Philip Wanjohi Nderitu (Lare) na Diwani wa Lanet/Umoja, Josphat Waweru Mwangi.

IMETAFSIRIWA NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

Wenger asema atarejea kutembea Arsenal ‘siku...

Polisi wazima mkutano wa Mudavadi mjini Mbale